• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Ruto adai kumiliki kura za eneo la Mlima Kenya

Ruto adai kumiliki kura za eneo la Mlima Kenya

Na STEVE NJUGUNA

NAIBU Rais William Ruto amepuuzilia mbali juhudi za kiongozi wa ODM Raila Odinga kupenya Mlima Kenya.

Dkt Ruto alisema kuwa tayari anamiliki eneo hilo lililo na wapiga kura wengi.

Dkt Ruto ameonekana kuwa kwenye njia panda kisiasa akijitahidi kudumisha ushawishi wake Mlima Kenya wakati huu ambapo Bw Odinga amezindua kampeni kali eneo hilo.

“Kuna watu wamejua leo ati kuna mlima na sasa wameanza kutafuta google map ili waanze kupanda mlima. Ningetaka kuwaambia kuwa mimi ndiye mwenye mlima,” alisema.

“Walipokuwa kwingineko, nilizuru mara kadhaa eneo hili, tukajenga barabara Mlima Kenya na kuanzisha miradi mingine ya maendeleo. Ninawakaribisha mlimani lakini wanapokuja acha wajue kwamba kuna wenyeji kwa mlima,” alisema Naibu Rais katika Shule ya Msingi ya Nyahururu DEB, Kaunti ya Laikipia.

Wakati huo huo, Dkt Ruto pamoja na wabunge wanaoegemea kambi yake walipuuzilia mbali mkutano uliofanyika kati ya kiongozi wa ODM na viongozi wa kibiashara kutoka eneo la Mlima Kenya.

“Kuna watu wanaoandaa mikutano Nairobi kupanga jinsi ya kuja kuuza mtu ambaye amegundua leo kwamba kuna mlima unaopatikana mahali fulani. Msiruhusu watu wengine wanaoandaa mikutano Nairobi kuja kuwafanyia uamuzi kuhusu ni nani atakayekuwa rais wenu mpya,” alisema.

Mbunge wa Mathira, Rigathi Gachagua alisema hawatampa nafasi Bw Odinga kuwashinda katika kinyang’anyiro cha urais.

“Vuguvugu la walalahoi haliwezi kuzimwa. Naibu Rais amekuwa sehemu ya jamii ya Mlima Kenya kwa miaka mingi sasa na katika muda huo, amegeuka kipenzi cha watu,” alisema.

You can share this post!

Dinamo anayochezea Mkenya Onsando kuwania shaba Ligi Kuu ya...

Atakubali mistari ya Raila?