Na MWANDISHI WETU
NAIBU Rais William Ruto, Jumamosi aliwataka Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga kuunga mkono azma yake ya kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2022.
Dkt Ruto alisema alipohudumu kama naibu kiongozi wa ODM alimuunga mkono Bw Odinga katika uchaguzi mkuu wa 2007, hatua iliyomsaidia kuteuliwa Waziri Mkuu.
Vile vile, alisema alimsaidia Rais Kenyatta kushinda urais kwa mihula miwili kwa tiketI ya chama cha Jubilee.
“Inasikitisha kuwa watu hawa wawili wamekuwa wakinishambulia licha ya kwamba niliwasaidia kupata nyadhifa hizo kubwa. Sasa nawaomba waniunge mkono ili niwezeshe Wakenya wa tabaka la chini kupata kazi na maisha mazuri,” Dkt Ruto akasema.
Alisema hayo mjini Awendo, Kaunti ya Migori alipokaribishwa na Gavana wa Kaunti hiyo, Bw Okoth Obado na viongozi wengine wa eneo hilo alipofika huko kuvumisha azma yake ya urais.
Dkt Ruto alitoa mchango wa Sh1 milioni kufadhili ujenzi wa Kanisa la Kiadventisti la Awendo Central, Sh1.4 milioni kwa makundi ya bodaboda na Sh500,000 kwa akina mama wafanyabiashara mjini Awendo kama hatua ya kupiga jeki makundi hayo.