• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 8:55 AM
Ruto, Raila wazidi kuzozana huku wakiambiwa wakae wazungumze

Ruto, Raila wazidi kuzozana huku wakiambiwa wakae wazungumze

WINNIE ATIENO NA WANDERI KAMAU

KIONGOZI wa Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya, Bw Raila Odinga, amepepeta zaidi wito wake wa maandamano ya raia wiki ijayo huku Rais William Ruto, akisisitiza hatatimiza matakwa ya upinzani.

Makabiliano yao yanaendelea huku vaadhi ya wazee wa jamii za Waluo na Wamaasai wakitana wawili hao wapatane.

Vilevile, Seneta wa Nairobi, Bw Johnson Sakaja, pia alitoa wito kwa serikali izingatie kuwaskiza viongozi wa upinzani.

Akiwa katika Kaunti ya Mombasa jana, Bw Odinga alidai kuwa, serikali sasa inataka kutumia baa la njaa kuwafaidi wafanyabiashara wachache watakaokubaliwa kuagiza vyakula kutoka nje ya nchi.
Kulingana na Bw Odinga, serikali ilitoa zabuni kwa wafanyabiashara kuleta nchini vyakula mbalimbali kwa madai kuwa wataondolewa ushuru ilhali bei ya bidhaa hizo ni ya juu kuliko kuzinunua humu nchini.
“Hiyo ndiyo biashara wanafanya kwa jasho la wananchi. Watatumia mabilioni kuleta bidhaa kutoka nje lakini bei itaenda juu zaidi. Hii ni sababu nyingine tunasema serikali hii lazima iende nyumbani,” akasema akiwa katika mkutano wa hadhara eneobunge la Likoni.
Muungano wa Wasagaji Nafaka (CMA), ulikuwa umethibitisha hakuna mwanachama wao yeyote ambaye amepewa idhini ya kuagiza vyakula bila ushuru hadi sasa. Hii iliibua maswali kuhusu waliopewa zabuni hiyo.
Awali, muungano wa Azimio ulikuwa umeipa serikali makataa ya siku 14 kutimiza matakwa kama vile kupunguza gharama ya mahitaji muhimu ya umma, kushirikisha vyama vyote vikuu katika mchakato wa kuteua makamishna wapya wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), na kufungua mitambo ya kompyuta zilizotumiwa kuhifadhi na kupeperusha matokeo ya uchaguzi wa urais wa mwaka uliopita, almaarufu kama sava.
Baada ya muda huo kukamilika juma lililopita, Bw Odinga alitangaza kutakuwa na maandamano makuu jijini Nairobi mnamo Februari 20, kuishinikiza serikali.
Jumapili alipuuzilia mbali ilani iliyotolewa na Waziri wa Usalama, Prof Kithure Kindiki, dhidi ya wananchi kuvamia sehemu zinazopewa ulinzi maalumu na serikali.
Hii ni ikizingatiwa kuwa, ishara za uwezekano wa maandamano kufanywa hadi katika Ikulu zilionekana kutoka kwa matamshi ya baadhi ya viongozi wa upinzani.
“Bwana Kindiki hujajua mimi ni nani. Wakati nilikuwa napigania demokrasia ulikuwa bado (mchanga). Huu uhuru ambao tuko nao sasa haukuwepo wakati ule. Unafaa utupigie saluti. Tulikuwa tunapigana na simba wenye meno na makucha. Tuling’oa simba meno na kucha akabaki simba kibogoyo kwa hivyo wewe wacha kututisha,” akasema.
Bw Odinga alikuwa ameandamana na wanasiasa wa ODM kutoka Pwani na maeneo mengine ya nchi, pamoja na vinara wenza wa Azimio akiwemo Bw Kalonzo Musyoka (Wiper), Bi Martha Karua (Narc-Kenya), miongoni mwa wengine.
Walionya polisi wasikubali amri ya kuvuruga maandamano yatakayofanywa na badala yake waunge mkono nia ya maandamano hayo.
“Wewe ofisa ukiona raia mpigie saluti. Tunakutetea kwa sababu pia wewe uko na shida kama wananchi wengine,” akasema Bi Karua.
Hapo jana, Rais William Ruto alisema kuwa hatakubali kushinikizwa na upinzani kuhusu vile ataiongoza nchi.
Akihutubu katika uwanja wa Kibugua, Kaunti ya Tharaka Nithi, Rais Ruto alimtaja Bw Odinga na washirika wake katika mrengo wa Azimio kama watu “wenye mazoea ya ukiukaji wa sheria”.
“Sitaiongoza nchi kwa kuzingatia matakwa na shinikizo ninazopewa na washindani wetu. Walijaribu kubadilisha uamuzi wa Wakenya katika ukumbi wa Bomas wakashindwa. Wakaelekea katika Mahakama ya Upeo lakini wakashindwa. Mnadhani wataweza kupitia maandamano?” akauliza.
Rais Ruto alikana madai ya Bw Odinga kuwa hakuzingatia sheria katika uteuzi wa Jopo Maalum la Kuteua Makamishna wa IEBC, akisema wanachama wa jopo hilo wanawakilisha taasisi zote zinazohitajika kisheria.
“Kazi ya Rais huwa si kuteua, bali kuidhinisha uteuzi wao na kuchapisha majina ya wanachama hao, kama yanavyowasilishiwa na taasisi husika. Wanachama wanawakilisha taasisi zote muhimu. Sijui nilivunja sheria wapi kwa kuidhinisha uteuzi wao,” akasema Rais Ruto.
Alikuwa ameandamana na naibu wake, Bw Rigathi Gachagua, ambaye alisema hakuna kiasi chochote cha vitisho kitakachokubaliwa kutatiza utekelezaji wa ajenda za serikali kuhusu maendeleo.
  • Tags

You can share this post!

Mwanagofu Kibugu ala Sh0.6 milioni Magical Kenya Open

Vijana Kilifi wahimizwa wawe mstari wa mbele kutoa maoni...

T L