NA WINNIE ATIENO
KINARA wa ODM Bw Raila Odinga amewataka magavana wa mrengo wa Azimio la Umoja One Kenya, kutokubali kumezwa na chama tawala United Democratic Alliance cha muungano wa Kenya Kwanza, kwa ahadi kwamba kaunti zao zitapata maendeleo kutoka kwa serikali ya Kitaifa.
Bw Odinga alisema ingawa ni haki ya magavana wa muungano wa upinzani kushirikiana na serikali hawafai kushawishiwa kujiunga nayo chama au muungano tawala kwa kuwa ni haki ya kaunti kupata sehemu ya rasilmali za serikali.
Waziri mkuu huyo wa zamani alisema kwamba viongozi wa Azimio hawafai kuomba rasilmali kutoka kwa serikali ya kitaifa kwa sababu ni haki ya kila kaunti kupata.
Akizungumza alipokutana na viongozi wa Azimio eneo la Pwani mnamo Ijumaa, Bw Odinga alionya kuwa chama tawala cha UDA kimeanza kunyemelea ngome za Azimio, akiwataka viongozi wa mrengo wake kusimama kidete na kutoshawishiwa na ‘vitu vidogo vidogo’.
Hata hivyo aliwatetea viongozi wa Azimio hasa magavana ambao hivi majuzi wamekuwa wakifanya kazi na serikali kuu, akisisitiza kuwa wamepewa idhini na chama chao.
Alitoa mfano wa Gavana wa Mombasa Abdulswamad Nassir ambaye amekuwa akiahidi kushirikiana na Rais William Ruto akisema hafanyi makosa.
“Wale wamemuona Gavana Nassir akishirikiana nao wasidhani amekuwa mmoja wao au amehama chama. Nassir amepewa idhini na kinara wa chama kufanya kazi na serikali kwa mujibu wa katiba,” alisema Odinga.
Magavana wengine wa Azimio ambao wameahidi kushirikiana na Rais Ruto ni Simba Arati( Kisii), Wavinya Ndeti( Machakos) Gidion Mung’aro(Kilifi), Glady’s Wanga( Homa Bay), Julius Malombe (Kitui) na Mutula Kilonzo Jnr( Makueni).
Bw Odinga aliwataka viongozi hao kutogeuka omba omba akisisitiza ni jukumu la serikali kuu kutoa fedha za ugatuzi kwa serikali za kaunti.
“Tunataka serikali kuu itoe pesa kwa serikali za kaunti ili wananchi wapate maendeleo na huduma. Ni jukumu la serikali kupeleka raslimali mashinani ili serikali za kaunti zipate rasilmali za kuhudumia wananchi,” alisema.
Alisema anajua njama ya viongozi wa serikali kulemaza chama cha ODM kwa kunyemelea wanachama wao walio uongozini.
“Unamwalika mtu nyumbani kwako anaongea na wewe lakini anamkonyezea mke wako macho. Anakuja lakini haji na madhumuni mazuri. Tuko katika muungano wa Azimio ni lazima Wiper, ODM, Jubilee, DP, Kanu iwe na nguvu ndio mrengo wetu uwe dhabiti. Watu wanasema nguvu ya ODM inadidimia Pwani, inaonekana adui anapenya penya akiingia ndani,” alisema Bw Odinga.
Alisema mwaka huu, ODM itasafisha chama chake ili kiwe na nguzu zaidi akiwataka wanachama wake wapendane, wafanye kazi kwa umoja na wakome kusengenyana akisema inaleta chuki kwenye chama.
Bw Odinga alisema licha ya chama tawala kunyakua kiti cha ubunge cha Nyali, ODM itaweka mikakati ili kikikomboe uchaguzi wa 2027.
Subscribe our newsletter to stay updated