• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Uamuzi wa mahakama wavuruga urithi wa Uhuru 2022

Uamuzi wa mahakama wavuruga urithi wa Uhuru 2022

Na WANDERI KAMAU

UAMUZI wa Mahakama Kuu kufutilia mbali Mpango wa Maridhiano (BBI) umevuruga handisheki na mikakati ya Rais Uhuru Kenyatta kuandaa urithi wake 2022.

Kulingana na wadadisi wa siasa, uamuzi huo uliotolewa Alhamisi, umemwacha Rais Kenyatta kwenye njiapanda, ambapo itabidi atathmini upya mwelekeo wake kisiasa kuanzia sasa.

Tangu Rais alipobuni handisheki na kiongozi wa ODM, Raila Odinga, mnamo 2018, mpango huo umekuwa ukifasiriwa na baadhi ya wakosoaji wake kama njama ya kumtengenezea njia kiongozi huyo kutwaa urais 2022.

Hata hivyo, hali ilibadilika katika siku za hivi karibuni, baada ya Rais Kenyatta kuonekana kuupendelea muungano wa One Kenya Alliance, unaowashirikisha kiongozi wa chama ANC, Musalia Mudavadi, Kalonzo Musyoka (Wiper), Maseneta Moses Wetang’ula (Ford Kenya) na Gideon Moi (Kanu).

Mdadisi wa siasa Javas Bigambo anasema kuna uwezekano mkubwa uamuzi huo “umeashiria mwisho wa handisheki na BBI.”

“Kile kilichowaunganisha Rais Kenyatta na Bw Odinga ni masuala hayo mawili kwa miaka mitatu ambao mchakato umekuwa machoni mwa Wakenya. Kuvurugika kwake kunamaanisha ukaribu wa kisiasa wa wawili hao umeisha, ikiwa hakutakuwa na nafasi yoyote kwa wale wanaoendesha mpango huo kuwasilisha rufaa mahakamani,” asema Bw Bigambo.

Anaeleza hilo pia litatoa nafasi kwa miungano mipya ya kisiasa kubuniwa, hasa miongoni mwa viongozi waliohisi kutengwa na mchakato huo.

“Tutashuhudia wanasiasa wakibuni miungano ya kisiasa kwa misingi ya ‘kulipiza kisasi’ kutengwa kwao katika mpango huo,” anasema.

Wanasema athari nyingine ni kuwa ushawishi wa Rais Kenyatta kama msemaji mkuu kwenye mchakato wa urithi utapungua sana.

“Wanasiasa walikuwa wakipigania kuwa karibu na Rais wakilenga kutangazwa kama warithi wake. Hilo ndilo lilikuwa lengo kuu la kubuniwa kwa One Kenya Aliance. Hali imebadilika. Itabidi aanze mkakati mpya ili kurejesha usemi wake tena,” asema mdadisi wa siasa Mark Bichachi.

You can share this post!

WANDERI KAMAU: Waliofanya KCSE wazingatie nidhamu kufaulu...

Kufanikisha refarenda sasa ni kama kushuka mchongoma