• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 4:55 PM
Uhuru ajaza nafasi nne za makamishna wa IEBC

Uhuru ajaza nafasi nne za makamishna wa IEBC

Na BENSON MATHEKA

Rais Uhuru Kenyatta jana aliteua watu wanne kujaza nafasi zilizokuwa wazi za makamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Rais Kenyatta aliwasilisha kwa bunge majina ya Bi Juliana Cherera, Bw Francis Mathenge Wanderi, Bi Irene Cherop Masit na Bw Justus Abonyo Nyang’aya ili wapigwe msasa na kuidhinishwa.

Wakipitishwa na bunge, wanne hao watajaza nafasi za makamishna waliojiuzulu.Watajaza nafasi zilizoachwa na Roselyne Akombe, Paul Kurgat, Connie Maina na Margaret Mwachanya waliojiondoa baada ya uchaguzi mkuu wa 2017.

Tangu kujiuzulu huko, IEBC imekuwa na makamishna watatu ambao ni mwenyekiti Wafula Chebukati, Profesa Yakub Guriye na Bw Boya Molu.

Wanne hao waliteuliwa kutoka kwa orodha ya watu 36 waliohojiwa na Jopokazi ya kuteua makamisha wa IEBC, ambalo liliongozwa na mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Nairobi, Dkt Elizabeth Muli.

Jopo kazi hilo lilipokamilisha mahojiano mwezi jana, Dkt Muli alisema kwamba zoezi hilo lilidhihirisha kuwa Kenya ina watu waliohitimu kuhudumia nchi yao.

Uteuzi wa wanne hao unajiri miezi miwili baada ya Mahakama Kuu kuamua kwamba bila kuwa na makamishna wote saba, shughuli za IEBC ni haramu.

Tume hiyo imekata rufaa dhidi ya uamuzi huo uliotolewa na majaji watano waliozima mchakato wa BBI.

Hatua ya Rais Kenyatta kuchukua hatua za kujaza nafasi za makamishna hao wanne zilionekana kuwa za kuokoa BBI na pia maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao ambao unahitaji tume kuwa imeundwa kikamilifu ili kuendesha uchaguzi kwa utaratibu uliowekwa kisheria.

You can share this post!

Mmoja auawa kwenye mzozo kuhusu vijana wawili

Kenya na TZ kurahisisha upimaji corona