• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Simbas yaomba Wakenya Sh40 milioni kujiandaa kwa mchujo

Simbas yaomba Wakenya Sh40 milioni kujiandaa kwa mchujo

Na Geoffrey AneneĀ 

SHIRIKISHO la Raga la Kenya (KRU) linahitaji Sh40 milioni kuiandaa Kenya Simbas kisawasawa kwa mchujo wa Kombe la Dunia utakaoandaliwa nchini Ufaransa kutoka Novemba 11-23, 2018.

Katika mahojiano na Taifa Leo mnamo Septemba 7, Mkurugenzi wa Raga wa KRU Thomas Odundo amesema KRU inatafuta fedha hizo zitakazogharamia matayarisho, kambi ya mazoezi na ziara ya Simbas mjini Marseille ambapo italimana na Canada, Hong Kong na Ujerumani.

Simbas, ambayo inanolewa na kocha kutoka New Zealand Ian Snook, imekuwa ikifanya mazoezi ya viungo katika jimu ya Alpha Fit kwenye barabara ya Ngong Road hatua chache kutoka makao makuu ya KRU jijini Nairobi.

Kila Ijumaa na Jumamosi, Simbas inafanya mazoezi hayo ya viungo kujiweka fiti. Inafanya mazoezi mepesi ya uwanjani kila Jumamosi. Itaanza mazoezi makali ya uwanjani Oktoba 1.

Inatarajia kusakata mechi mbili za kirafiki jijini Nairobi kabla ya kuelekea Marseille. Kenya imeomba Shirikisho la Raga Duniani (World Rugby) kuitafutia mechi ya kujipima nguvu dhidi ya Namibia, ambayo iko Kundi B katika Kombe la Dunia.

Namibia ilifuzu baada ya kupepeta Kenya, Tunisia, Morocco, Uganda na Zimbabwe katika Kombe la Afrika la Dhahabu lilokamilika Agosti 18.

Kenya ilifuzu kushiriki mchujo wa mwisho kwa kumaliza ya pili barani Afrika. Mshindi kati ya Kenya, Canada, Hong Kong na Ujerumani ataingia Kundi B linaloshirikisha Namibia, New Zealand, Italia na Afrika Kusini. Kombe la Dunia ni mwaka 2019 nchini Japan.

You can share this post!

Makocha wengi wang’ang’ania nafasi ya kunoa...

#KenyaVsGhana: Nyota watakaokosa mechi

adminleo