• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Utepetevu hospitalini KNH unavyomsababishia mama uchungu

Utepetevu hospitalini KNH unavyomsababishia mama uchungu

Na GEOFFREY ANENE

HOSPITALI ya Kitaifa ya Kenya (KNH) inamulikwa tena kwa madai ya kumfanyia mama mmoja upasuaji vibaya wakati wa kujifungua.

Susan Nekesa anasema alitembelea hospitali hii maarufu akihisi uchungu wa uzazi Januari 25 na kujifungua watoto wawili pacha siku iliyofuata.

Hata hivyo, saa chache baada ya upasuaji huo, tumbo lake lilivimba na akaanza kusikia maumivu makali.

Uchungu aliohisi, aliambia runinga ya Citizen, ulikuwa mbaya sana kiasi cha kumfanya asiongee.

Katika ripoti yake, Nekesa anajikokota kukaa kwenye kitanda chake, huku machozi yakimtoka.

Huku akilia, anasimulia kisa hicho akisema, “Naomba Mungu nisipoteze uwezo wangu wa kukumbuka.”

“Nilipokuja kumuona, nilipata amefura tumbo,” dadake Nekesa, Evelyn Anindo anasema.

“Tumbo lake pia lilikuwa moto sana na hakuwa anaweza kuzungumza. Tuliwasiliana kupitia ishara.”

Baada ya kulalamikia maafisa wa matibabu wa KNH, Nekesa alirudishwa katika chumba cha kufanyiwa upasuaji, na ni wakati huo madaktari walikiri walikuwa wamefanya kosa.

“Iligunduliwa kwamba upasuaji ulifanywa vibaya,” anasema Robert Sitati, bwanake Nekesa.

“Sehemu ya matumbo madogo, karibu sentimita 50, ilikuwa nje ya mahali inatakiwa kuwa,” anasema.

Kurekebisha hali hiyo, madaktari waliondoa sehemu iliyoathirika na kuacha mwanya mdogo (unaoitwa stoma) kumwezesha kupitisha uchafu kupitia mfuko maalum (colostomy).

Mgonjwa huyu pamoja na familia yake walisalia na matumaini kuwa atapata afueni na kurejea nyumbani na watoto hao pacha.

Ndani ya Hospitali Kuu ya Kenyatta. Picha/Hisani

Hata hivyo, familia ilipokea habari za kuhuzunisha Jumanne kwamba mtoto mmoja ameaga dunia.

“Walisema kwamba mtoto wangu alikuwa na shimo kwenye moyo wake,” anasema Nekesa kwa huzuni.

Hata hivyo, mumewe Nekesa anasema aliambiwa na mfanyakazi mmoja wa KNH kwamba mtoto wao alisongwa na maziwa.

“Mtu aliniambia kwamba mtu aliyekuwa akimpa mtoto wangu maziwa hakuwa na ujuzi,” Sitati anasema.

Kilichofuata masaibu ya Nekesa, ambaye anaomboleza kifo cha mtoto wake, ni kipindi cha huzuni, kutelekezwa na machungu dhidi ya madaktari wa KNH, ambao hawakufanya kazi yao vyema.

“Hakuna anayemshughulikia,” anasema Anindo.

“Mfuko huo maalum ukijaa, mzigo ni wake mwenyewe kujikokota hadi kwenye chumba cha kujisaidia kuufanya uwe tupu.”

Kwa wakati huu, familia yake imeshindwa la kufanya, huku hospitali hii ikiwaomba wawe na subira kwa sababu haina washauri wa kushughulikia Nekesa.

Mapema mwezi huu wa Machi, madaktari wanaojiongeza masomo waligoma baada ya wenzao kusimamishwa kazi kwa muda kutokana na upasuaji wa kichwa uliofanyiwa mgonjwa tofauti na yule alistahili kufanyiwa.

Sitati anasema hospitali hiyo imemuonya dhidi ya kuhamisha mke wake ikisema atalipia ada yote ya hospitali mwenyewe akiondoka KNH.

Nekesa anatumai siku moja atapata kuona watoto wake tena. “Wameniweka hapa kwa muda mrefu sana…Nimekuwa nikivumilia nikitumai kwamba siku moja nitaenda kuona watoto wangu,” anasema.

You can share this post!

KNH mashakani tena kufuatia upasuaji ovyo wa utumbo

Pigano la Okwiri na Ouma laahirishwa hadi Aprili 18

adminleo