• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Hali ya hatari nchini Ethiopia kudumu kwa miezi sita ijayo

Hali ya hatari nchini Ethiopia kudumu kwa miezi sita ijayo

Waziri wa Ulinzi nchini Ethiopia, Bw Siraj Fegessa. Picha/ Hisani

Na MASHIRIKA

HALI ya tahadhari iliyotangazwa nchini Ethiopia baada ya kujiuzulu kwa aliyekuwa waziri mkuu wa taifa hilo itadumu kwa miezi sita, amesema waziri wa ulinzi nchini humo.

Aidha, hilo linalenga kuzima maandamano ya kisiasa na shinikizo za uhuru wa kujieleza kutoka kwa vyama vya kutetea haki za binadamu.

Tangazo hilo lilitolewa kwa mara ya kwanza na shirika la habari la serikali, baada ya mkutano wa baraza la mawaziri mnamo Ijumaa.

Kulingana na serikali, hilo linajumuisha marufuku dhidi ya magazeti ama majarida yoyoye “yanayoweza kuwachochea raia ama kuzua migawanyiko ya kisiasa.”

“Lengo kuu la serikali ni kukabili uwezekano wowote wa kuzuka kwa mapigano. Hatutaki hali ambapo watu wanapoteza maisha yao bila sababu zozote,” akasema Waziri wa Ulinzi, Siraj Fegessa.

Aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo, Hailemariam Desalegm alijiuzulu mapema wiki iliyopita “ili kutoa nafasi kwa mwafaka wa kisiasa kupatikana.” Bw Desalegm pia alijiuzulu kama kiongozi wa chama tawala cha Ethiopian People’s Revolutionary Democratic Front (EPRDF).

Agizo hilo linatarajiwa kupitishwa na Bunge kwa muda wa siku 15 zijazo.

 

You can share this post!

Tobiko aanza kazi kwa kuonya wafanyabiashara haramu wakatao...

Watu 10 wanaswa kwenye msako dhidi ya karatasi za plastiki

adminleo