• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 4:48 PM
Shahbal aonekana kufaidika na siasa za kumrithi Joho

Shahbal aonekana kufaidika na siasa za kumrithi Joho

Na MOHAMED AHMED

SIASA za urithi wa kiti cha Gavana wa Mombasa Hassan Joho zimeonekana kuchukua mkondo tofauti ambao unaonekana kumfaidi mfanyabiashara Suleiman Shahbal ambaye anawinda kiti hicho mwaka 2022.?

Kufikia sasa, kiti hicho kimevutia wagombeaji kadha wakiongozwa na Bw Shahbal pamoja na mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir ambao ndio wameonekana kuwa washindani wa juu zaidi.

Wawili hao wote wanatarajia kupata kuidhinishwa na Bw Joho wakati uchaguzi huo utakuwa unakaribia mnamo 2022.? Licha ya Bw Joho kuonyesha dalili kuwa atamuunga mkono Bw Nassir, watu wake wa karibu ambao wamehusika katika mipango yake ya siasa wameonekana kuelemea upande wa Bw Shahbal, hatua ambayo inaibua masuali mengi kuliko majibu.

Miongoni mwa watu hao wa karibu wa Bw Joho ni washauri wa kisiasa wa gavana huyo akiwemo Rashid Bedzimba ambaye alikuwa mbunge wa Kisauni na aliyekuwa mshauri wa Bw Joho, Idriss Abdurahman ambaye sasa ni mshauri wa masuala ya usalama katika afisi ya gavana.

Bw Bedzimba ambaye ana ushawishi wa kutosha katika eneo bunge la Kisauni alipanga mkutano na viongozi wa kampeni zake na kuwakutanisha na Bw Shahbal.

Hatua hiyo ni baada ya kubainika kuwa Bw Abdurahman naye ndiye aliyechukua uongozi wa mipango ya kampeni ya Bw Shahbal.? Kwa upande Bw Bedzimba analenga kumkusanyia Bw Shahbal kura za Kisauni kulingana na ufuasi alionao.

Bw Bedzimba amehudumu eneo bunge hilo kwa zaidi ya miaka 15 kama diwani na mbunge.? Hata hivyo, mwaka 2017 alipoteza kiti hicho kwa mbunge wa sasa Ali Mbogo ambaye kwa sasa analenga kiti cha ugavana.

Aliyekuwa seneta wa Mombasa Hassan Omar pia analenga kiti hicho.? Siku za hivi karibuni, ni Bw Shahbal na Bw Nassir ambao ndio wameonekana kuzunguka zaidi kuuza sera zao mapema kwa wananchi.

Akizungumza katika ukumbi wa Sheikh Zayed eneo la Bombolulu baada ya kukutana na wafuasi hao wa Bw Bedzimba, Bw Shahbal alisema kuwa ana matumani kuwa kushikana na Bw Bedzimba kutamuezesha kunyakua kiti hicho cha ugavana.

Alisema pamoja watapigana na changamoto za utovu wa usalama, utumizi wa dawa za kulevya miongoni mwa vijana na ukosefu wa kazi.

“Nataka kumshukuru Bw Bedzimba kwa nafasi hii ya kunikutanisha na majemedari wake. Mimi nawaomba tushikane mkono ili tuhudumie watu wetu wa Kisauni na Mombasa kwa jumla tukiwa pamoja,” akasema Bw Shahbal.

Bw Bedzimba kwa upande wake alisema kuwa ameaumua kumuunga mkoni Bw Shahbal kwa sababu miongoni mwa wale wote ambao wanataka kuwania kiti hicho yeye yupo mbele.

Alimtaja Bw Shahbal kuwa kiongozi mwenye maono na mwenye azma ya kuhudumia wakazi wa Mombasa kwa hali na mali..? ? ? “Mimi madhali alikuja akaniomba anataka kukutana na nyinyi nikasema tumpe nafasi. Kwa sababu hata tukiangalia kwa wote wale ambao wanataka kiti hicho Bw Shahbal yupo mbele yao tayari,” akasema Bw Bedzimba.

Hayo yalijiri huku mbunge wa Mvita Bw Nassir akionekana kuondeleza siasa zake katika maeneo bunge ya Kisauni, Nyali na Changamwe.? ? ? Bw Nassir amekuwa akifanya mikutano na kujipigia debe ili apate nafasi hiyo baada ya kumaliza hatamu yake kama mbunge wa Mvita.

Aidha, mbunge wa Kisauni Ali Mbogo naye ameonekana kushikilia siasa za mashinani ambapo amekuwa akiendesha kampeni zake za kiti cha ugavana.

Ikiwa imesalia zaidi ya mwaka mmoja, wandani wa masuala ya siasa wanatazama iwapo wale ambao wameanza mapema siasa zao watatoboa hadi mwisho wa ushindani huo wa mwaka 2022.

Hii pia ni kwa sababu inatarajiwa kuwa kutaibuka wawaniaji wengine katika kumezea mate kiti hicho.? ? Ikisubiriwa hilo, kwa sasa viongozi waliopo wamepata wasaa wa kujipigia debe na kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kupata kiti hicho ifikapo mwaka wa uchaguzi.

You can share this post!

Ujanja wa Uhuru na Raila kuzima sauti zinazokosoa BBI

UGAVANA NAIROBI: Margaret Wanjiru alivyogeuka mwiba kwa...