• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 6:50 AM
UGAVANA NAIROBI: Margaret Wanjiru alivyogeuka mwiba kwa UhuRaila

UGAVANA NAIROBI: Margaret Wanjiru alivyogeuka mwiba kwa UhuRaila

Na CHARLES WASONGA

NI rasmi sasa kwamba uchaguzi mdogo wa ugavana wa Nairobi utafanyika Februari 18 kama ilivyotangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Hii ni baada ya Mahakama Kuu Jumanne jioni kudinda kuzuia tume hiyo kuchapisha notisi kuhusu tarehe ya zoezi hilo na masharti yanayopasa kuzingatiwa na wagombeaji na vyama vyama vitakavyowadhamini.

Aliyekuwa Gavana wa Nairobi Mike Sonko, kupitia wakili Wilfred Nyamu, alitaka mahakama izuie IEBC kuanzisha mchakato wa kujaza nafasi ya ugavana Nairobi hadi kesi hiyo itakaposikizwa na kuamuliwa.

Alidai sheria ilikiukwa katika hatua zote za kumtimua; kuanzia Bunge la Kaunti ya Nairobi hadi Seneti. Sasa macho yote yanaelekezwa kwa kinyang’anyiro hicho hasusan wagombeaji watakaodhaminiwa na mirengo mikuu ya kisiasa nchini; Handisheki na Tangatanga (au Team Hustler).

Mrengo wa handisheki unashirikisha Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga huku ule wa Tangatanga unaongozwa na Naibu Rais William Ruto ambaye anapania kuingia Ikulu 2022 bosi wake atakapostaafu.

Duru ziliambia jarida la ‘Jamvi la Siasa’ kwamba mrengo wa Jubilee unaongozwa na Rais Kenyatta unapania kutwaa kiti hicho kwa usaidizi wa ODM, kwa moyo wa handisheki.

Chini ya mpango huo, Jubilee itatoa mgombeaji huku ODM ikitoa mgombeaji mwenza, ilivyofanyika wakati wa uchaguzi wa Spika Benson Mutura mnamo Agosti .

Bw Mutura aliungwa mkono na madiwani wa ODM huku Jubilee “ikirudisha mkono” kwa kuunga mkono Diwani wa Baba Dogo Geoffrey Majiwa kutwaa wadhifa wa Naibu Spika.

Wale ambao wanapigiwa upatu kudhaminiwa na mrengo wa Rais Kenyatta na Odinga ni aliyekuwa Mbunge wa Dagoretti Kusini Dennis Waweru na aliyekuwa Mbunge wa Gatanga Peter Kenneth.

Mchanganuzi wa masuala ya kisiasa na uongozi Steve Ogolla naye amependekezwa kuwa mgombeaji mwenza wa atakayeteuliwa kupeperusha bendera ya Jubilee.

Wengine wanaodaiwa kumezea mate kiti hicho kilichosalia wazi baada ya maseneta kuidhinisha hoja ya kumtimu Sonko mamlakani ni aliyekuwa Karani wa iliyokuwa Baraza la Jiji la Nairobi Philip Kisia, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na mfanyabiashara wa Nairobi Agnes Kagure.

Lakini kile ambacho kimewatia mrengo wa handisheki tumbojoto uamuzi wa mrengo wa Tangatanga kumdhamini aliyekuwa Mbunge wa Starehe Askofu Margaret Wanjiru kuwa mgombeaji wake kwa tiketi ya chama chochote kile au hata kama mgombeaji mwenza.

Na kinasemekana kuwakosesha usingizi wapanga mikakati wa kundi la handisheki usingizi na dalili kwamba Askofu Wanjiru, ambaye pia aliwahi kuhudumu kama Waziri Msaidizi wa Nyumba, atapigwa jeki na gavana aliyetimuliwa Mike Mbuvi Sonko.

Kando na kuwa meaneja shupavu mwanasiasa mkakamavu, kiongozi huyo wa Kanisa la Jesus Is Alive Ministries (JIAM) anayo tajriba ya kuwahi kung’ang’ania kiti cha ugavana wa Nairobi 2017 aliposhiriki mchujo wa Jubilee lakini akabwagwa na Sonko.

Isitoshe, kando na ushawishi alio nao kama kiongozi wa kidini, uungwaji mkono atakaoupata kutoka kwa Dkt Ruto, wabunge wa mrengo wa Tangatanga kutoka Nairobi na maeneo mengine utaboresha nafasi yake ya kutwaa kiti hicho.

Kati ya wabunge 17 wa Nairobi mrengo wa wale waliegemea Tangatanga ni watano; James Gakuya (Embakasi Kaskazini), John Kiarie (Dagoreti Kusini), George Theuri (Embakasi Magharibi), Nixon Korir (Langata), James Gathiru (Embakasi ya Kati).

Wabunge tisa wanaegemea mrengo wa handisheki huku Charles Kanyi (Starehe), Nancy Gakuya (Kasarani) na Waihenya Ndirangu (Roysambu) hawajajinasibisha na mrengo wowote.

Wadadisi wa kisiasa wanasema kuwa Wanjiru na Sonko wataupa mrengo wa handsheki kibarua kigumu zaidi ikizingatiwa kuwa wawili hao wako na ufuasi mkubwa zaidi katika mitaa ya mabanda.

“Ikumbukwe Wanjiru na Sonko wamewahi kuwakilisha maeneo bunge ya Nairobi ambako kuna mitaa mikubwa ya mabanda ambao wakazi wao ndio hujitokeza kwa wingi kupiga kura haswa katika chaguzi ndogo. Wanjiru aliwakilisha Starehe ambayo inajumuisha mtaa wa mabanda wa Mathare, Kiamaiko na Huruma huku Sonko aliwakilisha vitongoji kama Mukuru Fuata Nyayo alipohudumu kama Mbunge wa Makadara na alipata kura nyingi zaidi katika mitaa mingine yenye wakazi wengi alipowania kiti cha useneta na ugavana wa Nairobi. Kundi la handisheki lina kila sababu ya kuhofia wanasiasa kama hawa,” akasema Bw Martin Andati ambaye ni mchanganuzi wa masuala ya kisiasa.

“Ikiwa Rais Kenyatta na Raila hawatapanga kampeni zao vizuri huenda wakapokonywa kiti cha ugavana wa Nairobi walivyopokonywa kiti cha ubunge cha Msambweni na vile vya udiwani vya wadi za Lakeview (Nakuru) na Gitugi (Murang’a),” anaongeza.

Huku akitiwa shime na hamasa na ushindi alioundikisha katika majuzi dhidi ya mgombeaji aliyeungwa mkono na Rais Kenyatta na Bw Odinga (Bw Omar Boga) katika eneo bunge hilo lililoko kaunti ya Kwale, Dkt Ruto anatarajiwa kumwaga wandani wake Nairobi katika jitihada zake za kutwaa kiti hicho.

“Msukumo wa Ruto katika kuwasilisha mgombeaji katika kiti cha ubunge cha Msambweni licha ya chama chake kujiondoa ulikuwa ni kupima kama angali na ushawishi katika eneo la Pwani. Hatachelea kurudia mtihani huo huo katika kaunti ya Nairobi yenye maeneo bunge 17 na zaidi ya wapiga kura milioni mbili kutoka jamii zote nchini. Amefanya chaguo bora la kumuunga mkono Askofu Wanjiru mwenye tajriba na uzoefu katika siasa za Nairobi,” anasema mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Javas Bigambo.

Lakini Mbunge wa Makadara George Aladwa anasema kuwa Askofu Wanjiru sio tisho kwa Uhuru na Raila, akisema kuwa mwanasiasa huyo alishindwa na aliyekuwa Gavana wa Nairobi Evan Kidero 2017.

Bw Aladwa, ambaye ni mwenyekiti wa ODM kaunti ya Nairobi, anasema mrengo wa handisheki una ushawishi mkubwa katika kaunti ya Nairobi ilivyodhihirika wakati wa shughuli ya ukusanyaji wa saini za kuunga mkono mswada wa marekebisho ya Katiba kupitia mpango wa maridhiano (BBI).

“Ikiwa tuliweza kupata zaidi ya sahihi 500,000 kutoka Nairobi licha ya kundi la Tangatanga wakiongozwa na Ruto (Naibu Rais) kupinga, nini kitatuzuia kuwabwaga katika uchaguzi mdogo Februari 18, 2021?” akauliza mwanasiasa huyo ambaye amewahi kuwa Meya wa Nairobi.

Lakini wakili Danstan Omari anatofautiana na kauli ya Aladwa akisema ushawishi wa Rais Kenyatta na Odinga umeshuka zaidi haswa miongoni mwa wapiga kura kutoka jamii ya Wakikuyu ambao ndio wengi Nairobi.

“Kura za Wakikuyu zimemwendea Dkt Ruto ambaye ameanzisha mpango wa kuwasaidia vijana na akina mama kibiashara maarufu kama “Hustler Movement”.

Nao wapiga kura kutoka jamii ya Waluhya ambao wamekuwa wakifaidi kutoka kwa mradi wa “Sonko Rescue Team” watafuata mkondo ambao Sonko atawaelekeza.” anasema Bw Omari ambaye pia ni mchanganuzi wa masuala ya kisiasa.

Lakini Mbunge Maalum Maina Kamanda anasema wapiga kutoka jamii za Waluhya, Kisii na Luo wataunga mkono mgombeaji wa handisheki walivyofanya katika uchaguzi mdogo wa Kibra mnamo Oktoba mwaka jana.

Hata hivyo, inakisiwa kuwa huenda Dkt Ruto akajipata pabaya endapo atajitokeza waziwazi kumuunga mkono Askofu Wanjiru wakati ambapo chama chake, Jubilee, kitakuwa kimedhamini mgombeaji wake.

Naibu Rais ndiye Naibu Kiongozi wa chama hicho tawala.Kwa hivyo, ataonekana kumkaidi kiongozi wa chama chake na bosi wake katika serikali ya Jubilee, hali ambayo inaweza kuchochea shinikizo za kutaka akitimuliwe kupitia hoja bungeni.

Ikumbukwe kuwa mwezi Juni mwaka huu Rais Uhuru Kenyatta alishinikiza kutimuliwa kwa wandani wa Dkt Ruto wote walioshikilia nyadhifa za uongozi katika Seneti na Bunge la Kitaifa, pamoja na kamati za mabunge hayo.

Ilidaiwa kuwa viongozi hao wakiongozwa na aliyekuwa kiongozi wa wengi katika Seneti Kipchumba Murkomen na mwenzake aliyeshikilia wadhifa huo katika bunge la kitaifa Aden Duale, walikaidi misimamo na maongozi ya Jubilee ndani ya nje ya bunge.

You can share this post!

Shahbal aonekana kufaidika na siasa za kumrithi Joho

Kura ya Matungu kipimo cha umaarufu wa Mudavadi