• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Walevi wakesha waumini wakilala

Walevi wakesha waumini wakilala

Na WAANDISHI WETU

WANANCHI wengi wanaopenda vileo walikiuka maagizo ya kukaa nyumbani usiku wa kuamkia jana Ijumaa, na badala yake wakaendelea kuburudika vilabuni hadi asubuhi kuukaribisha mwaka mpya.

Licha ya serikali kusisitiza kuwa sharti la kukaa nyumbani kuanzia saa nne usiku ili kuepusha maambukizi ya corona bado liko, uchunguzi wa Taifa Leo ulibainisha walevi wengi walipuuza hayo.

Kwa upande mwingine, makanisa yalitii agizo hilo na kufanya ibada zao za kuukaribisha mwaka mpya mapema kabla saa za kafyu na waumini wakarudi makwao.

Katika eneo la Nakuru Mashariki, Wateja katika kilabu cha Platinum 7D Lounge walikuwa miongoni mwa wanywaji pombe ambao waliendelea kuburudika hadi wakakaribisha mwaka mpya bila kujali kama wangekamatwa.

Kamanda wa polisi Ellena Kabukuru alisema maafisa wake walikamata magari matano na watu kadhaa waliokiuka kafyu mjini Nakuru mkesha wa mwaka mpya.

Katika Kaunti ya Murang’a, watu wengi walikuwa nje baada ya saa nne usiku licha ya polisi kushika doria.

“Leo naona kazi ni ngumu kiasi… Hata wenzetu wengine wamehepa kazi na wako kwa baa. Itabidi tufunge macho kiasi watu warukishe mwaka,” afisa mmoja aliambia Taifa Leo mjini Kiria-ini.

Hali ilikuwa sawa na hiyo katika miji ya Kangari, Thika, Kangema, Kenol, Sagana, Maragua, Kabati na Kamahuha ambapo watu walijifungia ndani ya baa kujificha, lakini wakapiga fujo za kukaribisha mwaka mpya ilipogonga saa sita usiku.

Mjini Elburgon, Kaunti ya Nakuru, Taifa Leo iligundua kwamba watu walikuwa wakitembea barabarani na wengine wakiwa ndani ya baa wakilewa.

Hali sawa na hii ilishuhudiwa katika Kaunti za Kwale na Taita Taveta ambako watu walikesha wakikwepa polisi kusherehekea mwaka mpya.

Baadhi ya wanaoishi karibu na mpaka walivuka hadi Tanzania kusherehekea hadi asubuhi.

Katika kaunti ya Kisumu, makanisa yaliandaa ibada kati ya saa kumi na saa mbili usiku ili kuruhusu waumini kufika nyumbani kabla ya saa za kafyu kuanza.

Kanisa katoliki mjini Kisumu liliagiza makanisa yake yote kumaliza ibada saa mbili usiku.

Mjini Eldoret Kaunti ya Uasin Gishu, waumini walianza kumiminika katika makanisa yao saa kumi na moja jioni kwa ibada ya kuvuka mwaka ili kuepuka kukamatwa kwa kukiuka maagizo ya kutotoka nje.

Mchungaji Job Simiyu wa Fountain of Wisdom Chapel Eldoret alitoa changamoto kwa Wakenya wote kusahau changamoto za 2020 na kukumbatia uaminifu ili kuruhusu uponyaji wa nchi yao.

Katika kaunti ya Mombasa Askofu Tom Arati wa Bible Way Ministries Bishop aliandaa ibada kupitia mtandao na kuwahimiza Wakenya wasiwe na woga mwaka huu.

Ripoti za Eric Matara, Mwangi Muiruri, John Njoroge, Rushdie Oudia, Titus Ominde, Anthony Kitimo Na Wachira Mwangi

You can share this post!

Macho yote kwao 2021

Mikasa ya kufa maji yatamatisha 2020