• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 4:48 PM
FAUSTINE NGILA: Madikteta wasiruhusiwe kutumia mitandao wanavyotaka

FAUSTINE NGILA: Madikteta wasiruhusiwe kutumia mitandao wanavyotaka

VIONGOZI madikteta hawapendi ukweli, hasa ikiwa ukweli huo unaenezwa kupitia mitandao ya kijamii ambapo watu wengi hukita kambi katika muda wao wa ziada.

Mwezi huu tumejionea rais anayeondoka wa Amerika Donald Trump akizimiwa akaunti zake zote katika Twitter, Facebook na YouTube kwa kila kampuni hizo zilitaja kama matumizi ovyo ya majukwaa hayo kuwapotosha wananchi.

Akiendelea kusisitiza kuwa kulikuwa na wizi wa kura uchaguzini hata baada ya kuzimwa mitandaoni, rabsha ambazo zilitokea baada ya Bw Trump kuwaagiza wafuasi wake kuvamia bunge zilisababisha vifo vya watu watano.

Juzi, katika nchi jirani ya Uganda, ambapo Rais Yoweri Museveni alifanya Uganda taifa la kwanza duniani kulipa ushuru wa mitandao ya kijamii, Twitter na Facebook zilipigwa marufuku katika muda wote wa kabla, wakati na hata baada ya uchaguzi.

Mataifa haya mawili, ambayo yana misingi tofauti ya kisiasa na kiuchumi, lakini yanayotawaliwa na madikteta yameonyesha jinsi haki za wananchi zinaweza kukandamizwa kwa mbinu tofauti.

Kwa kuwa mitandao hiyo ya kijamii inamilikiwa na kampuni za Amerika, Bw Trump aliyahitaji majukwaa hayo zaidi ili kufikia wafuasi wake zaidi ya milioni 87.

Lakini akazimwa kutokana na ukomavu wa demokrasia nchini humo.Kinaya nchini Uganda ni kuwa, kwa kuona maandamano ya wafuasi wa chama cha Republican nchini Amerika, tume inayosimamia mawasiliano iliagiza intaneti izimwe wakati wa kura “ili tusishuhudie mauaji kama yale ya Amerika kutokana na maandamano.”

Kwa kuweka giza la mitandaoni, wananchi hawakuweza kutoa taarifa za moja kwa moja kuhusu visa vya udanganyifu au kulazimishwa na jeshi kupiga kura kama alivyodai mwaniaji urais Bobi Wine.L

akini Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya alivyojaribu kumpongeza Bw Museveni kwa ushindi wake kupitia Facebook, ujumbe huo ulifutwa kutokana na kile kampuni hiyo iliona uchaguzi haukuwa huru kwani Bw Museveni aliagiza intaneti izimwe.

Wiki chache tu kabla ya intaneti kuzimwa Uganda, serikali iliitaka kampuni ya Google kuondoa akaunti zote za YouTube ambazo zilikuwa zinaeneza jumbe za kukashifu serikali.

Google ilidinda kufuata agizo hilo.?Facebook, kwa upande wake, iliondoa video nyingi tu zilizopigia debe kampeni za Bw Museveni ikisema ni “mwenendo usiofaa”.

Ukaidi huo ulioneka kumkera sana Rais huyo ambaye sasa ataongoza Uganda kwa miaka 40, na akaamua kuondoa mawimbi ya intaneti.? Hii inaonyesha uwezo mkubwa wa mitandao uliochangiwa na teknolojia ambapo watu wengi walio na simu za kisasa wanapenda kutoa maoni yao ya kukosoa serikali au kutetea mwaniaji wao.

Lakini viongozi walio mamlakani baada ya kugundua hilo, sasa wanatumia mitandao hiyo kwa manufaa yao wenyewe, hasa wakati wa uchaguzi ambapo mihemko ya kisiasa hushuhudiwa.

Kwa demokrasia iliyokomaa, matumizi ya mitandao kwa wanasiasa yanafaa kuwa na uwajibikaji, na wananchi wanapotoa hisia zao wanafaa kusikizwa na wala si kufungiwa nje.

Hata hivyo, kwa wanasiasa wanaopenda kutumia mitandao hiyo kupotosha wananchi kwa kueneza chuki na uongo, wazimwe.

You can share this post!

MAUYA OMAUYA: Bobi Wine ameweka msingi, mapambazuko...

CHARLES WASONGA: Museveni amesaidia Uganda licha ya utawala...