• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Man-United wadengua Liverpool katika Kombe la FA na kufuzu kukutana na West Ham kwenye raundi ya tano

Man-United wadengua Liverpool katika Kombe la FA na kufuzu kukutana na West Ham kwenye raundi ya tano

Na MASHIRIKA

BAO la Bruno Fernandes kupitia frikiki ya dakika ya 78 liliwasaidia Manchester United kuwapepeta Liverpool 3-2 kwenye mechi ya raundi ya nne ya Kombe la FA mnamo Jumapili uwanjani Old Trafford.

Liverpool ndio waliopigiwa upatu wa kushinda mechi hiyo baada ya Mohamed Salah kufuta juhudi za awali za Mason Greenwood na Marcus Rashford waliowaweka Man-United katika dakika za 26 na 48.

Vikosi hivyo vilikuwa vikivaana kwa mara nyingine wiki moja baada ya kuambulia sare tasa kwenye gozi la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) uwanjani Anfield.

Dalili zote zikiashiria kwamba timu hizo zingetoshana nguvu kwa mara nyingine, Fernandes alitokea benchi na kuzidisha kasi ya mashambulizi ya Man-United na presha kutoka kwa masogora hao wa kocha Ole Gunnar Solskjaer ilimfanya Fabinho kumkabili Edinson Cavani visivyo nje ya kijisanduku cha penalti.

Fernandes aliyesajiliwa na Man-United kutoka Sporting CP ya Ureno kwa kima cha Sh6.6 bilioni mnamo Januari 2020, alimwacha hoi kipa Alisson Becker dakika 12 kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa mechi kupulizwa.

Ushindi wa Man-United unawapa tiketi ya kuchuana na West Ham United katika raundi ya tano ya Kombe la FA msimu huu. Ni mchuano utakaomkutanisha kocha David Moyes wa West Ham na waajiri wake wa zamani, Man-United, uwanjani Old Trafford.

Liverpool walishuka dimbani kwa minajili ya mchuano huo wakipania kusajili ushindi wa kwanza kutokana na mechi saba zilizopita katika mashindano yote. Mara ya mwisho kwa Liverpool wanaofunzwa na kocha Jurgen Klopp kushinda mechi ni Disemba 19 ambapo waliwapepeta Crystal Palace 7-0 katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) uwanjani Selhurst Park.

Chini ya Klopp, Liverpool ambao ni mabingwa watetezi wa EPL, sasa wamekosa kushinda mechi yoyote kati ya tano zilizopita ligini na wametandaza jumla ya michuano minne bila kufunga bao.

Kichapo cha 1-0 kutoka kwa Burnley mnamo Januari 21, 2021 kinamaanisha kwamba ushindi wa pekee ambao umesajiliwa na Liverpool mwaka huu wa 2021 ni ule wa 4-1 waliovuna dhidi ya makinda wa Aston Villa kwenye raundi ya tatu ya Kombe la FA mnamo Januari 8 ugani Villa Park.

Hadi walipoangushwa na Burnley, Liverpool walikuwa wakijivunia rekodi ya kutoshindwa katika jumla ya mechi 68 za EPL kwenye uwanja wao wa nyumbani wa Anfield.

Baada ya chombo chao kuzimwa na Man-United ya kocha Ole Gunnar Solskjaer, mechi tano kati ya sita zijazo ambazo Liverpool watasakata ligini zitakuwa dhidi ya vikosi vinavyoshikilia nafasi saba za kwanza kufikia sasa jedwalini.

Masogora hao wa Klopp watafunga mwezi huu wa Januari dhidi ya Tottenham Hotspur na West Ham United kabla ya kupepetana na Brighton, Manchester City na Leicester City kwa usanjari huo. Baada ya kuwaendea RB Leipzig ya Ujerumani kwenye mkondo wa kwanza wa raundi ya 16-bora ya Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Februari 16, Liverpool watawaalika Everton ugani Anfield kabla ya kuchuana na Sheffield United uwanjani Bramall Lane.

Kushindwa kwa Liverpool uwanjani Old Trafford mnamo Jumapili usiku kunamaanisha kwamba kikosi hicho cha Klopp kimefaulu kusonga mbele kwenye Kombe la FA baada ya raundi ya nne mara moja pekee mnamo 2019-20.

Kwa upande wao, Man-United hawajawahi kukosa kutinga hatua ya robo-fainali za Kombe la FA tangu 2013-14.

Rekodi mbovu ya Liverpool ilichangia motisha ya Man-United walioshuka dimbani wakijivunia ushindi wa 1-0 dhidi ya Watford kwenye raundi ya tatu ya Kombe la FA msimu huu.

Katika mashindano yote ya hadi kufikia sasa msimu huu, Man-United wamepoteza mechi moja pekee kati ya 13 zilizopita tangu wabanduliwe mapema kwenye gozi la UEFA.

Walijibwaga ugani dhidi ya Liverpool wakiwa na kiu ya kuendeleza ubabe uliowashuhudia wakitoka nyuma mnamo Januari 20 na kupokeza Fulham kichapo cha 2-1 katika EPL uwanjani Craven Cottage. Ushindi huo uliwawezesha kuwaruka tena Leicester na Man-City na kurejea kileleni mwa jedwali kadri wanavyopania kutia kibindoni taji la 21 la EPL muhula huu wa 2020-21.

Licha ya rekodi nzuri katika misimu ya hivi karibuni kwenye mapambano ya kuwania mataji mbalimbali isipokuwa UEFA, Man-United wametia kapuni Kombe la FA mara moja pekee katika kipindi cha miaka 16 iliyopita.

Man-United kwa sasa wanajiandaa kuvaana na Sheffield United katika EPL mnamo Januari 27 ugani Old Trafford huku Liverpool wakiwaendea Tottenham siku moja baadaye.

Man-United kwa sasa wamewabandua Liverpool kwenye Kombe la FA mara 10. Aidha, Liverpool wameshinda mechi moja pekee kutokana na 15 zilizopita katika mashindano yote ugani Old Trafford. Kikosi hicho kimepoteza mechi 10 na kuambulia sare mara nne na hakijawahi kushinda mechi yoyote kutokana na nane zilizopita uwanjani Trafford.

Man-United wameshinda kila mojawapo ya mechi zao nane zilizopita za Kombe la FA nyumbani huku Liverpool wakiwa mabingwa watetezi wa kwanza wa taji la EPL kubanduliwa mapema katika raundi ya nne ya Kombe la FA baada ya Man-City mnamo 2014-15.

You can share this post!

Wazee Lamu washauri wanaume waache kutumia kiholela dawa za...

UDAKU: Neymar hapoi! Sasa amejinasia kidege Emilia wa...