Na CHARLES WASONGA
WABUNGE kadhaa wa Nairobi pamoja na Seneta Johnson Sakaja Alhamisi walifika katika bunge la kaunti hiyo kuwapa shime madiwani wapitishe Mswada wa BBI.
Viongozi hao walikuwa; George Aladwa (Makadara), Babu Owino (Embakasi Mashariki), Maina Kamanda (Mbunge Maalum) na aliyekuwa Mbunge Mwakilishi wa Nairobi Rachel Shebesh.
Mswada huo ulipitishwa na madiwani waliokuwa ukumbini Alhamisi majira ya alasiri na kuifanya Nairobi kuwa kaunti ya hivi punde kuidhinisha marekebisho hayo ya Katiba.
Jumla ya madiwani 114 walipiga waliokuwepo walipiga kura ya ndio, moja kwa moja, ilhali wenzao wanne walipiga kura ya NDIO kupitia mitandaoni.
Ni madiwani wawili pekee ambao hawakushiriki upigaji kura kuhusu Mswada huo ambao unapendekeza jumla ya mageuzi 73 kwa Katiba ya sasa iliyozindulia mnamo 2010.
Hoja ya kuhusu Mswada huo iliwasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Haki na Masuala ya Kisheria Diwani Joseph Komu na kuungwa mkono na mwenzake Kennedy Obura.
Nairobi sasa inaungana na orodha ya kaunti ambazo zimepitisha mswada huo; ambazo ni, Siaya, Kisumu, Homa Bay, Kajiado, West Pokot Magharibi, Busia, Trans Nzoia, Vihiga, Laikipia na Kisii.