• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:55 AM
‘Kilio cha wanafunzi chuoni Moi kitafutiwe suluhu’

‘Kilio cha wanafunzi chuoni Moi kitafutiwe suluhu’

Na LYDIA OMAYA

MALALAMISHI ya njaa miongoni mwa wanafunzi katika vyuo vikuu humu nchini yamezidi hawa katika Chuo Kikuu cha Moi.

Wamekuwa wakidhihirisha hali yao mtandaoni kwa njia ya ‘memes’ ambayo wengi wanachukulia kuwa mzaha tu.

Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Vyuo (HELB) inalaumiwa pakubwa kusababisha hali hii chuoni Moi.

Wanafunzi wanadai kuwa fedha hizo zimecheleweshwa kwao tu kwani wanafunzi wengine wameshapokea mikopo.

Wana hofu kwamba hali hii huenda ikasababisha wengi kukosa mtihani wao kutokana na ukosefu wa karo. Tatizo la njaa tayari linashuhudiwa.

Wanafunzi wanaoathirika zaidi ni wale wanaoishi katika mabweni ya chuo.

Tangu kupika ipigwe marufuku chuoni Moi, wanafunzi wengi wamepata taabu kutafuta nyumba za kukodisha nje ya shule lakini sio wote wanaobahatika kutokana na ukosefu wa kodi maanake kupangisha ni bei ghali huenda wasiweze kulipa.

La pili ni kuwa nyumba ni chache na zile ambazo ziko mbali na shule ndizo za kodi nafuu ya kama Sh12,000 kwa muhula mmoja. Lakini itamlazimu kutumia nauli kila siku kuingia chuoni na baadaye kurejea chumbani.

Kutoruhusiwa kupika katika mabweni ya chuoni basi kunawalazimu kununua vyakula katika hoteli za shule na hata nje ya shule ambazo zinauza vyakula kwa bei wasioweza kumudu kwa muda mrefu.

“Tangu kupika shuleni kupigwe marufuku, wanafunzi wanaoishi mle wanateseka sana kwa kulazimika kutumia si chini ya Sh150 hotelini na mikahawani kila siku. Hapo awali hali ilikuwa afadhali kwa sababu wengi wangebeba vyakula kutoka nyumbani vya kupika kwa angalau muhula mmoja na hivyo basi pesa zingetumika kidogo,” alisema mwanafunzi wa mwaka wa nne Dan (sio jina lake halisi).

Mara kwa mara vyakula huisha kwa hizi hoteli na basi kulazimika kushinda njaa. Ni jambo la kushangaza kuwa wanafunzi wanazirai kutokana na njaa.

“Wanafunzi wengine wanazirai kwa kukaa siku nyingi bila chakula chochote. Mara mingi nyakati za usiku ambulensi inasikika ikichukua mwanafunzi ambaye ameathirika ili apelekwe hospitalini. Ni hali ya kuhuzunisha sana.” Cynthia Ainga ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa tatu anayeishi kwenye bweni anaeleza.

Mkuu wa Maslahi ya Wanafunzi – Dean – John Ayieko ametoa wito kwa wanafunzi wanaoathirika na njaa kujitokeza kupitia kwa vinara na viongozi wa wanafunzi ili kupata usaidizi.

Baadhi ya wanafunzi wanatoa ombi waruhusiwe kupika shuleni tena.

Ni muhimu HELB kutoa mikopo hiyo ya fedha baada ya wanafunzi hawa kuandamana mjini Eldoret, Jumanne. Huenda hali ikazidi kuwa mbaya ikiwa malalamishi haya hayatatiliwa maanani.

Lydia Omaya ni mtafiti

You can share this post!

Wakili John Bwire Ajitokeza Kudhamini Mashindano ya Soka...

Mashabiki wa Samidoh sasa wamshauri ajichunge asipake tope...