• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:55 PM
Mashabiki wa Samidoh sasa wamshauri ajichunge asipake tope umaarufu wake

Mashabiki wa Samidoh sasa wamshauri ajichunge asipake tope umaarufu wake

Na SAMMY WAWERU

MWANAMUZIKI wa Mugithi, Samuel Muchoki maarufu kama Samidoh ameendelea kupongezwa na mashabiki wake mitandaoni baada ya kuweka wazi kuhusu mpango wake wa kando ulioishia kujaaliwa mtoto.

Juma lililopita, Bw Samidoh alifichua kwamba amekuwa kwenye uhusiano haramu na mwanasiasa mmoja wa jiji la Nairobi.

Kwenye chapisho Facebook, msanii huyo ambaye pia ni afisa wa polisi, alikiri uhusiano wake na Karen Nyamu uliishia kujaaliwa mtoto.

“Ni kweli nilikuwa kwenye uhusiano na Bi Karen Nyamu, uhusiano ambao ulisababisha kuzaliwa kwa mtoto asiye na hatia. Nimekuwa nikisaidia mwanangu na nitaendelea kumsiadia. Ninajivunia kuwa baba wa watoto wangu,” Samidoh akaelezea, akiomba familia yake msamaha na mashabiki wake katika kile alitaja kama “kuwaweka katika hali mbaya”.

Huku akieleza kutoridhishwa na video ambayo Nyamu alipakia mitandaoni, Samidoh akionekana kukumbatia mtoto huyo wa kiume na kucheza naye, alisema hajawahi kuacha mke wake wa miaka 11 kwenye ndoa kwa sababu ya mwanamke mwingine.

Mke wake ametambulika kama Edith Nderitu. “Nilimuomba msamaha na pia familia yangu…Ninakiri makosa yangu na ambayo ninajutia…” mwanamuziki huyo akaendelea kueleza.

Ni hatua ambayo imeendelea kuridhisha mashabiki wake, wengi wakielekeza hisia zao mitandaoni.

“Kuwa imara rafiki yangu Samidoh. Nina imani Eddy (mkewe, Edith Nderitu) atapata nafasi moyoni mwake kukusamehe. Ninakupongeza kwa kusimama kidete na familia yako,” #Collins Wanderi akachangia kwenye chapisho hilo lenye zaidi ya michango 69, 000.

“Umebarikiwa, ndoa yako haitasambaratika,” Esther Muthoni Ndirangu akasema.

Wengi wa waliotoa mchango na kupongeza staa huyo kwa ujasiri wake kukiri kuwa na mpango wa kando, walikuwa wanawake kwa mujibu wa majina yao.

“Mwanamume jasiri na komavu hukiri makosa yake na kuomba msamaha. Ninakuheshimu!” #Alice W Wamwea akaelezea.

Akiridhia msamaha wa Samidoh, Shiku Mwari wa Kinyanjui alieleza kufurahishwa kwake na hatua hiyo, huku akihimiza wanaume wengine wanaojipata katika hali hiyo kuiga nyayo zake.

Licha ya kongole chungu nzima alizopokea, baadhi walizua utani.

“Samidoh usijali. Ukichunga mke wako wa kwanza, Mungu atakujaalia mwingine,” #Mungai Gathogo akachangia.

Bi Karen Nyamu ambaye pia ni wakili, kwenye mahojiano na mtangazaji tajika Felix Odiwour, maarufu kama Jalango, kupitia runinga yake ya You-Tube, Jalango TV, aliomba mke wa Samidoh msamaha akisema wakati walipojuana hakujua ni mume wa wenyewe.

“Niligundua wakati maji yalikuwa yameshamwagika,” Karen akajitetea.

Aidha, alisema walijuana mwaka wa 2019.

  • Tags

You can share this post!

‘Kilio cha wanafunzi chuoni Moi kitafutiwe...

Uwanja maarufu wa Maracana nchini Brazil sasa kuitwa Rei...