• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 12:30 PM
Uchunguzi waanzishwa kufuatia kifo cha mfanyabiashara Thika

Uchunguzi waanzishwa kufuatia kifo cha mfanyabiashara Thika

Na MWANGI MUIRURI

IDARA ya polisi imeanzisha uchunguzi kufuatia kifo cha mfanyabiashara mmoja Thika, ambapo mwili wake ulipatikana akiwa nusu uchi kwenye gari lake katika egesho la magari, Kaunti Ndogo ya Gatanga.

Kulingana na ripoti iliyoandikishwa na mke wa mfanyabiashara huyo aliyetambulika kama Samuel Murigi katika kituo cha polisi cha Kaunti Ndogo ya Gatanga, aliondoka nyumbani kwake mtaa wa Landless, kiungani mwa mji wa Thika Machi 13, kuhudhuria hafla ya mchango wa rafikiye Kenol, kilomita 16 kutoka wanakoishi.

Hakurejea nyumbani, hatua ambayo ilishinikiza mke wake, Bi Catherine Nduta kuandikisha ripoti ya mtu aliyetoweka.

Alisema aliingiwa na wasiwasi baada ya kumpigia simu, mwanamke akaipokea na kueleza walikuwa pamoja katika eneo la burudani.

Aliambia maafisa wa polisi kwamba aliamua kuenda eneo hilo, Jogoo Kimakia Country Club, kuthibitisha ikiwa alikuwepo.

“Nilitembelea baa hiyo na gari lake aina ya Toyota double cabin pickup lenye nambari za usajili KAQ 553 P, lilikuwa katika egesho la magari,” ripoti ya Catherine inaelezea.

Kulingana naye, alipolikagua aliona mwili wa mume wake.

Mkuu wa Polisi Gatanga, Peter Muchemi aliambia Taifa Leo Dijitali kwamba uchunguzi utategua kitendawili cha maafa ya mfanyabiashara huyo.

“Hatuna uhakika alivyokumbana na mauti. Tunafuatilia nyayo na nyakati zake za mwisho. Tutatoa taarifa tukipata mwelekeo,” akasema afisa huyo.

Uchunguzi utabaini iwapo alikuwa Kenol kuhudhuria hafla ya mchango, alivyopatikana katika baa na alikuwa na kina nani.

Aidha, upasuaji wa maiti utafichua kilichosababisha kifo cha mfanyabiashara huyo.

“Tukipata mwelekeo tutajua iwapo ni kisa cha kujiondoa uhai, kuuawa au kifo cha kawaida,” Bw Muchemi akasema.

Afisa huyo alisema tayari faili ya kesi hiyo imefunguliwa katika Idara ya Uchunguzi wa Jinai (DCI). Mkuu wa DCI eneo hilo, Bw John Kanda, alisema matokeo ya kwanza yatatolewa Jumatano.

“Tumekagua eneo la mkasa na kukusanya sampuli zitakazofanyiwa uchunguzi. Kwa sasa, tunashughulikia mashahidi watakaoandikisha taarifa. Upasuaji wa mwili ukifanyika, tutajua hatua tutakayochukua,” Bw Kanda akasema.

Mfanyabiashara huyo alikuwa amewekeza katika nyumba za kukodi, uchukuzi na uuzaji wa bidhaa.

Mwenyekiti wa Jamii ya Wafanyabiashara Thika, Bw Alfred Wanyoike amemuomboleza mwendazake, akimtaja kama mfanyabiashara milionea aliyekuwa na bidii.

TAFSIRI: Sammy Waweru.

You can share this post!

Mhudumu wa afya afariki baada ya kuchanjwa Astra Zeneca

Hit Squad kuelekea Congo Ijumaa