• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 2:13 PM
LEONARD ONYANGO: Handisheki itakufa baada ya refarenda

LEONARD ONYANGO: Handisheki itakufa baada ya refarenda

Na LEONARD ONYANGO

MVUTANO uliopo baina ya chama cha ODM na baadhi ya maafisa serikalini kuhusu Mswada wa Mpango wa Maridhiano (BBI), ni ithibati kwamba mpango huo ulikuwa na njama fiche ambayo si kuunganisha Wakenya jinsi tumekuwa tukiambiwa.

Viongozi wa ODM, wakiongozwa na Seneta wa Siaya James Orengo na wabunge Otiende Amollo (Rarieda) na Junet Mohamed (Suna Mashariki), hivi karibuni walitishia kususia BBI.

Walidai kuwa Mswada huo ‘umenyakuliwa’ na baadhi ya watumishi serikalini na wanalenga kuutumia kutafuta mrithi wa Rais Uhuru Kenyatta baada ya 2022.Baadaye walitueleza kwamba Rais Kenyatta na kinara wa ODM, Raila Odinga, walifanikiwa kutatua utata uliokuwepo.Ni miaka mitatu sasa tangu kuanza kwa mchakato wa BBI.

Rais Kenyatta na Bw Odinga wamekuwa wakituambia kwamba malengo yao kuwa na mwafaka wa maridhiano, almaarufu handisheki, ni kuunganisha Wakenya na kumaliza vurugu ambazo zimekuwa zikishuhudiwa nchini kila baada ya uchaguzi.Lakini matukio ya hivi karibuni yameweka wazi kwamba mpango wa BBI unalenga siasa za urithi za 2022.

Jambo la wazi kabisa ambalo limejitokeza ni kwamba Rais Kenyatta na Bw Odinga wanalenga mambo tofauti, licha yao kuonekana kusukuma BBI kwa pamoja.Kuna uwezekano kwamba ukuruba baina ya Rais na kinara huyo wa ODM utaisha baada ya Wakenya kupitisha BBI.

Vile vile, kuna uwezekano kwamba baada ya kura ya maamuzi ya kurekebisha Katiba kukamilika, Rais Kenyatta ataweka wazi jina la mtu atakayemuunga mkono kumrithi katika Uchaguzi Mkuu 2022.

Seneta wa Baringo Gideon Moi, kiongozi wa chama cha Amani National Congress (ANC) Musalia Mudavadi na kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka watakuwa kwenye kikosi hicho.Inaonekana mswada wa BBI umebuni nyadhifa za kuhakikisha kuwa kila mmoja wa vigogo hao katika orodha ya urithi, atajipatia kiti.

Kwa upande mwingine, kuna hatari ya Bw Odinga kuachwa mpweke. Inaonekana kinara huyo alitarajia kwamba Rais Kenyatta angemuidhinisha kuwa rais katika uchaguzi ujao, lakini mambo huenda yakamwendea upogo.

Hata hivyo, karata ya Rais yaweza kutibuka iwapo Bw Odinga ataamua kuungana na Naibu Rais William Ruto. Hapo basi mwaniaji atakayeungwa mkono na Rais Kenyatta atakuwa na kibarua kigumu kupambana na kikosi ngangari kitakachojumuisha Dkt Ruto na Bw Odinga.

You can share this post!

Uchumi, sanaa na desturi za kabila la Wadigo uswahilini

Serikali yasema itaondoa barabarani matatu zionazokaidi...