• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 11:13 AM
Mreno aliyetuma droni kwa makazi ya Ruto ashtakiwa

Mreno aliyetuma droni kwa makazi ya Ruto ashtakiwa

Na MWANGI MUIRURI

Mtalii aliyekamatwa Machi 29 kwa madai ya kutuma droni ya ujasusi hadi katika makao rasmi ya Naibu wa Rais Dkt William Ruto mtaani Karen ameshtakiwa.

Bw Piotrukasz Litwiniuk ambaye ni raia wa Ureno alishtakiwa kwa makosa manne ambayo ni kuingiza droni hiyo nchini bila kibali kinachohitajika, kuitumia nchini bila idhini inayohitajika, kuihudumu bila kujisajili na pia kukosa kuisajili droni hiyo–makosa yanayokaa mzunguko wa barabara.

Kwa kina, upande wa mashtaka ulielezea mahakama kwamba muundo wa droni hiyo ni Mavic Air2 yenye utambulisho MA2UE3W na ambayo iliingizwa nchini January 7 kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Moi Jijini Mombasa.

Alikiuka sheria za Kenya kwa kuitumia Machi 29 akiwa jirani wa Dkt Ruto na ambapo walinzi waliokuwa wakiwajibikia Usalama wa makazi hayo waliiona angani na wakaifuatilia hadi kuiona ikirejea bomani mwa Mreno huyo.

Mama Rachel Ruto akiwa ndiye bibiye Naibu wa Rais ndiye aliripoti kisa hicho katika kituo cha polisi cha Hardy ambapo timu ya Uchunguzi wa Jinai ilitumwa kupeleleza zaidi.

Mbele ya Hakimu Martha Mutuku wa mahakama ya Milimani, Litwiniuk alikanusha mashtaka hayo na akaachiliwa na bodi ya Sh200,000 pesa taslimu au mdhamini wa Sh500,000, kesi ikitengwa kusikizwa kwa wiki mbili zijazo.

You can share this post!

Hatimaye serikali yaungama chanjo ya AstraZeneca ina madhara

Familia 3,000 zaagizwa kuhama Mto Ngong