• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 10:08 PM
Mvamizi Hassan analenga magoli yasiyopungua 15 kikosini Bandari

Mvamizi Hassan analenga magoli yasiyopungua 15 kikosini Bandari

Na ABDULRAHMAN SHERIFF

KIUNGO mshambuliaji wa Harambee Stars, Abdalla Hassan, analenga kutinga mabao 15 na zaidi msimu huu wa Ligi Kuu nchini (FKF), akitumai michezo itarejea tena baada ya kusitishwa kwa mara nyingine sababu ya virusi hatari vya corona.

Akizungumza na Taifa Leo jana Jumapili, mchezaji huyo wa Bandari FC ambaye amefungia timu ya taifa Harambee Stars mabao matatu, amesema anajitahidi kutimiza shabaha hiyo.

Hassan alifunga dhidi ya Taifa Stars ya Tanzania, Misri na Togo.

“Najizatiti kuhakikisha natinga mabao angalau 15 kwa timu yangu ya Bandari kufikia mwisho wa msimu huu wa 2020-2021. Lengo ni kujinoa zaidi na pia kusaidia timu yangu kufanya vyema ligini ili kumaliza katika nafasi mojawapo za juu,” alieleza.

Tayari amechangia mabao tisa – amefunga matano na kutoa pasi zilizozalisha manne.

“Natamani ligi kuu irudi ili nitimize shabaha yangu,” akaongeza.

Kiungo huyo alisema anajihisi kuwa katika hali nzuri na hivyo anatarajia kuendelea kuwika uwanjani wakati soka itaruhusiwa kuendelea.

“Kama timu hatukuanza vizuri ligi msimu huu lakini taratibu tumeimarika na kushika mwendo. Tamaa yangu kubwa ni kwamba tutafanya vizuri hata zaidi.”

Vile vile, anatazamia kutumia makali yake kuwezesha Stars kufana katika mechi za kufuzu kwa makala yajayo ya Kombe la Dunia 2022 nchini Qatar.

You can share this post!

Ruth kidedea akiweka rekodi mpya ya dunia mbio za 21km

Inter Milan yaanza kunusia taji la Serie A