• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 12:58 PM
Uhuru ashauriwa kuiga Kibaki

Uhuru ashauriwa kuiga Kibaki

Na TITUS OMINDE

ASKOFU Mkuu wa Kanisa Katoliki, Dayosisi ya Eldoret, Dominic Kimengich amemtaka Rais Uhuru Kenyatta kuiga njia ambayo ilitumiwa na rais mstaafu Mwai Kibaki katika kushughulikia ukuaji wa uchumi bila kukopa.

“Wakati wa siku za Mzee Kibaki, mikopo ya kigeni ilikuwa midogo sana. Tulikuwa tunatumia raslimali zetu zilizopo hapa nchini kukuza uchumi wetu. Ni bora twende polepole kwenye masuala ya kukopa na kusimamia uchumi wetu,” alisema Askofu

Akiongea baada ya kulisha familia zaidi ya 300 za barabarani mjini Eldoret wakati wa kuadhimisha Jumatatu ya Pasaka, Askofu Kimengich alisema kuendelea kwa serikali kukopa zaidi kutafanya Kenya kuwa mtumwa wa wakopeshaji.

Askofu Kimengich alieleza kuwa ufisadi na usimamizi mbaya wa rasilimali zilizopo ndio chanzo cha Kenya kukopa kila mara.

Alisema mwenendo wa kukopa zaidi umeiweka nchi katika hali mbaya kwani pesa nyingi zilizokopwa hazina manufaa kwa raia wa kawaida kwa sababu ya ufisadi.

“Utamaduni wa kukopa zaidi umeiweka nchi yetu katika hali ya kutatanisha. Pesa nyingi zilizokopwa hazifaidi nchi kwa sababu ya ufisadi na usimamizi duni wa uchumi,” akasema Askofu Kimengich.

“Natoa wito kwa serikali kuwa na uangalifu sana. Ikiwa tunaendelea kukopa ni nani atakayelipa madeni haya? Hatupaswi kuwaachia watoto wetu mzigo kama huu wa madeni. Serikali inapaswa kwenda polepole kwenye suala la kukopa,” akaongeza.

You can share this post!

ODM yaenda kortini kupinga matokeo ya kura za Matungu

Mkopo wa IMF wazua hasira kwa Wakenya