• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 6:50 AM
Visa vya wizi wa ng’ombe vyazidi Gatundu Kaskazini

Visa vya wizi wa ng’ombe vyazidi Gatundu Kaskazini

Na LAWRENCE ONGARO

WAKAZI wa vijiji vya Ngorongo na Kairi, Gatundu Kaskazini, wameachwa na hofu baada ya mifugo yao kuibwa.

Wakazi hao walieleza ya kwamba mnamo Jumatano ng’ombe wapatao wanane waliibwa majira ya usiku.

Bi Hellen Nyambura alisema ng’ombe wake wawili waliibwa mnamo Jumatano usiku.

Alieleza kuwa wezi hao, anashuku, ni watu hutoka mbali ambao walikuwa wamejihami kwa silaha hatari.

“Hata ng’ombe wangu mmoja alikuwa na ndama wake lakini pia aliibwa kutoka zizini,” alisema Bi Nyambura.

Naye Peter Ngige mkazi wa kijiji cha Kairi alisema wanashuku wengi wa wafanyakazi wa vibarua wa kazi za shamba katika maeneo hayo ndio pengine wanashirikiana na watu fulani ili kutekeleza wizi huo.

Alieleza kuwa wezi hao hupuliza dawa nyumbani kwa wenye ng’ombe zao halafu wanatekeleza wizi huo.

“Tunaitaka serikali kuingilia kati na kufanya uchunguzi mkali ili kubainisha kiini cha wizi huo kuenea bila mtu yeyote kutiwa nguvuni,” alifafanua Bw Ngige.

Wakazi hao wanaitaka serikali kuingilia kati kuona ya kwamba wezi hao wanakabiliwa vilivyo na kutiwa nguvuni.

Wanadai kuwa wizi huo unatekelezwa usiku wakati wa kafyu na kwa hivyo wanataka maafisa wa usalama wapige doria katika vijiji hivyo.

Tukio hilo limewaacha wakazi hao na hofu tele huku wengi wao wakiwaweka ng’ombe wao ndani katika nyumba zao.

Naye Gabriel Kimani wa kijiji cha Ngorongo alisema wezi hao wanaingia kwa boma kwa ujasiri majira ya usiku.

“Sisi kama wakazi wa eneo hilo tunashindwa kuelewa jinsi hasa wezi wanavyotembea usiku na ni wakati wa kafyu. Serikali ichukue hatua haraka kabla hawajatumalizia mifugo yetu,” alisema Bw Kimani.

Alieleza kuwa hata mbwa wanaofugwa vijijini huwa hawabweki ambapo wanashuku wezi hao hutumia dawa za kupuliza.

  • Tags

You can share this post!

Supamaketi zina kibarua kudhibiti msongamano wa watu...

Huduma za ukaguzi magari kutekelezwa kila Ijumaa mjini...