• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:50 AM
JAMVI: Ukimya uliogubika OKA ni ishara mbovu, Uhuru amewaacha mataani?

JAMVI: Ukimya uliogubika OKA ni ishara mbovu, Uhuru amewaacha mataani?

Na CHARLES WASONGA

MASWALI yameibuka kufuatia ukimya wa vinara wa muungano wa One Kenya Alliance (OKA) miezi miwili baada ya wao kuchangamsha ulingo wa kisiasa kufuatia ushindi wao katika changuzi ndogo katika maeneo bunge Matungu, Kabuchai na kiti cha useneta wa Machakos.

Hii ni licha ya kwamba vinara hao; Musalia Mudavadi (ANC), Kalonzo Musyoka (Wiper), Moses Wetang’ula (Ford Kenya) na mwenyekiti wa KANU Gideon Moi kunasibisha ushindi wagombeaji wao katika chaguzi hizo na mwanzo wa safari ya kuwezesha mmoja wao kuingia Ikulu 2022.

“Watu wa Matungu, Kabuchai na Machakos sasa wametupa motisha kubwa zaidi. Ushindi huu umetupa nafasi ya kuanza rasmi safari ya kwenda Ikulu. Wale wanaolalamika umoja wetu ndio nguvu yetu,” Bw Mudavadi akawaambia wanahabari baada ya ushindi wa Seneta Agnes Kavindu Muthama katika uchaguzi mdogo wa useneta wa Machakos uliofanyika Machi 18.

Awali, muungano huo ulivuna ushindi katika chaguzi ndogo za maeneo bunge ya Matungu (Kakamega) na Kabuchai (Bungoma) zilizofanyika Machi 4, kupitia Peter Oscar Nabulindo (ANC) na Majimbo Kalasinga (Ford-Kenya), mtawalia.

Ilidaiwa kuwa baraka za Rais Uhuru Kenyatta zilichangia ushindi huo, lengo likiwa kuzima nyota za kisiasa za Naibu Rais William Ruto na kiongozi wa ODM Raila Odinga, haswa katika eneo la magharibi. Chama cha ODM, kupitia katibu mkuu Edwin Sifuna, kilidai kushindwa kwa ODM katika eneo bunge la Matungu kulichochewa na serikali.

Isitoshe, ni baada ya matokeo hayo ambapo Seneta wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo, ambao hadi wakati huo walikuwa watetezi sugu wa Bw Odinga, walidai Katibu katika Wizara ya Usalama Karanja Kibicho alikuwa akiendesha njama ya kuzima azma ya kiongozi huyo wa ODM kuingia Ikulu 2022.

Mbw Orengo na Amollo walidai kuwa “serikali inapanga kuunga mkono mmoja wa vinara ya One Kenya Alliance 2022” ilhali wao sio wadau katika handisheki kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga.

Lakini tangu, Aprili 1, Rais Kenyatta alipoandamana na Bw Odinga kukagua miradi ya wa ujenzi wa kituo cha kisiasa cha magari ya uchukuzi cha Green Park, Nairobi na barabara kadha katika kaunti ya Kajiado, shughuli zimefifia ndani ya muungano wa One Kenyatta.

Kando na kufanya mikutano miwili katika makazi ya Bw Kalonzo na Bw Wetang’ula, siku tofauti, vinara hao wamekomesha mtindo wao wa kutoa taarifa kwa wanahabari kila mara huku wakimpiga vita Bw Odinga.

Hata hivyo, duru ziliambia Taifa Jumapili kuwa kando na hisia kuwa Rais Kenyatta “amerejelea ukuruba kati yake na Bw Odinga” kumeibuka vuta nikuvute kati ya vyama hivyo kuhusu nani kati ya vinara hao anafaa kuungwa mkono kama mgombeaji urais kwa tiketi ya OKA.

You can share this post!

NASAHA ZA RAMADHAN: Mwenyezi Mungu hurehemu na kusamehe...

Korti yafungua miradi ya mabilioni ya pesa Pwani