• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Pasta atozwa Sh2,000 baada ya kufumaniwa na muumini

Pasta atozwa Sh2,000 baada ya kufumaniwa na muumini

Na SHABAN MAKOKHA

PASTA wa Kanisa la ADC eneo la Lugari, Kaunti ya Kakamega, ametozwa faini ya ng’ombe, kondoo na Sh2,000 baada ya kufumaniwa akiwa uchi akishiriki vya haramu na mke wa muumini wake.

Mhubiri huyo kwa jina Samuel amepokezwa adhabu hiyo na baraza la wazee wa jamii ya Kabras alipopatikana na hatia ya kushiriki mahaba na mke wa Charles Mulongo kwenye kitanda chao cha ndoa katika kijiji cha Mufutu usiku wa Ijumaa.

Pesa hizo zitatumika kutakasa boma la Bw Mulongo ili familia yake isikumbwe na nuksi ya usherati.

Pia kikao cha wazee hao kiliidhinisha talaka kati ya Bw Mulongo na mkewe aliyekiri kuwa alifurahia ustadi wa mhubiri huyo kitandani baada ya Bw Mulongo kumtelekeza.

Bw Mulongo ana wake wawili na alikuwa akilala katika nyumba ya mke wake wa pili, mhubiri huyo alipokuwa kitandani na mkewe.

“Tumemtoza mhubiri huyo faini ya kondoo, ng’ombe na Sh2,000 ambazo zitatumika kuandaa tambiko la kutakasa boma la Bw Mulongo,” akasema Mzee wa kijiji hicho Saulo Ambani baada ya kikao cha kusuluhisha kesi hiyo.

Akigusia kisa chenyewe, Bw Mulongo alisema kuwa ni kitendo ambacho hakukitarajia kwa kuwa alikuwa anaheshimu Bw Samuel ambaye amekuwa akitoa mafunzo kemkemu kanisani.

“Niliitwa na watoto wangu kisha wakanieleza mwanaume aliye uchi alikuwa amepatikana kwenye chumba cha mama yao. Nilikimbia na kufika chumbani, nikashtuka kupata alikuwa mhubiri katika kanisa langu. Amekuwa akitufundisha kanisani tuwapende wake wetu na tusiwaruhusu wawili waliounganishwa na Mungu watenganishwe na binadamu. Inasikitisha kuwa alitenda kitendo hiki na mke wangu tena kwenye kitanda chetu cha ndoa,” akasema Bw Mulongo.

Mwanawe mkubwa wa kiume naye alisema kuwa dada yake ndiye aliyempasha habari kuwa mhubiri huyo alikuwa akijienjoy na mamake.

Mtoto huyo pia hulala katika nyumba hiyo.

“Nilikimbia na kumpata akiwa uchi katika kitanda chetu. Alijaribu kupigana nami lakini nikamlemea na hata alipoponyoka na kukimbia, nilimfuata ndipo akaokolewa na majirani,” akasimulia.

Kufuatia tukio hilo, Bw Mulongo amewahamisha watoto wake kutoka nyumba hiyo hadi tambiko lifanywe na pia kutalikiana na mkewe.

“Hata kama mwanamke amekukosea heshima kivipi. Ni makosa makubwa kumleta mwanamume katika kitanda chenu cha ndoa. Hili ni jambo lisilovumilika,” akasema.

Alifichua kuwa pasta huyo amekuwa akija kwake mara kwa mara na hakukoma hata baada ya kuonywa mara kadhaa na watoto wake.

Tukio linajiri baada ya mwanamume anayefanya kazi Nakuru kurejea nyumbani ghafla na kumpata mkewe mjamzito na jiraniye katika kijiji cha Makuyu eneobunge lilo hilo mnamo Februari 18, 2021.

You can share this post!

Majonzi 18 wakifa ajalini

FUNGUKA: ‘Mapenzi mtandaoni…raha!