• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
JAMVI: ‘Baba’ anajua kwamba UhuRuto wanamkata miguu kule Nyanza?

JAMVI: ‘Baba’ anajua kwamba UhuRuto wanamkata miguu kule Nyanza?

Na LEONARD ONYANGO

RAIS Uhuru Kenyatta na Naibu wa Rais William wameanza mchakato wa kutaka kumlemaza kisiasa kiongozi wa ODM Raila Odinga katika eneo la Nyanza.

Huku Rais Kenyatta akilenga kumpokonya Bw Odinga udhibiti wa maeneo ya Kisii na sehemu ya Kaunti ya Migori, Naibu wa Rais Ruto analenga kunyakua vigogo wa ODM na wasomi kutoka maeneo ya Luo Nyanza.

Rais Kenyatta, kupitia kwa Waziri wa Usalama Fred Matiang’i, analenga kudhihirisha ubabe wake kupitia uchaguzi mdogo wa Bonchari ambapo vyama vya ODM na Jubilee vimesimamisha wawaniaji.

Chama cha Jubilee kimesimamisha mbunge wa zamani wa Bonchari Zebedeo Opore huku aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kawi nchini (EPRA) Mhandisi Pavel Oimeke akipeperusha bendera ya ODM kwenye uchaguzi huo mdogo utakaofanyika Jumanne.

Hii ni mara ya kwanza kwa ODM na Jubilee kushindana kwenye chaguzi ndogo tangu Rais Kenyatta na Bw Odinga kuafikiana kushirikiana, almaarufu handisheki, mnamo 2018.Chama cha ODM kimekuwa kikishutumu Jubilee kwa kutumia maafisa wa polisi kuhangaisha viongozi wake wanaoendesha kampeni za Bw Oimeke.

Alhamisi, polisi walivamia nyumbani kwa Gavana wa Kisii James Ongwae – anayeongoza kampeni za ODM katika eneobunge la Bonchari – na kufukuza Seneta wa Kisii Profesa Sam Ongeri, Mwakilishi wa Kike Kisii Bi Janet Onge’era na mwenzake kutoka Migori Bi Pamela Odhiambo waliomtembelea.

Polisi walidai kuwa viongozi hao walikuwa wakifanya mkutano kinyume na marufuku ya kufanya mikutano ya kisiasa iliyotolewa na siasa kuzuia maambukizi ya virusi vya corona.Chama cha ODM pia kinadai kuwa serikali imekuwa ikitumia machifu na wazee wa Nyumba Kumi kupigia debe Bw Opore.

“Chama cha ODM ni lazima kishinde uchaguzi mdogo wa Bonchari ili kudhihirisha kwamba Bw Odinga angali anadhibiti kisiasa eneo la Kisii. Iwapo chama cha Jubilee kitashinda, ujumbe utakuwa kwamba ODM imepoteza umaarufu,” anasema Bw Mark Bichachi, mdadisi wa masuala ya kisiasa.

KUHANGAISHA ODM

Wadadisi wa masuala ya kisiasa pia wanasema kuwa hatua ya polisi kuhangaisha viongozi wa ODM katika eneobunge la Bonchari ni ishara kwamba uhusiano baina ya Rais Kenyatta na Bw Odinga tayari umesambaratika.

Baadhi ya viongozi wa Jubilee waliambia Jamvi kuwa Rais Kenyatta pia analenga Kaunti ya Migori iliyo na maeneobunge manane.Wakazi wa maeneobunge ya Kuria Magharibi na Kuria Mashariki zimekuwa zikipiga kura upande wa serikali.

Rais Kenyatta pia analenga kuvutia upande wake Gavana Okoth Obado aliye na idadi kubwa ya wafuasi katika Kaunti ya Migori.Kwa upande mwingine, ujumbe wa Naibu Rais Ruto ukiongozwa na Eliud Owalo, ulikutana na viongozi mbalimbali wa ODM pamoja na wasomi kutoka Nyanza.

Viongozi hao walikutana katika Hoteli ya Hermosa jijini Nairobi.Miongoni mwa waliohudhuria kikao hicho ni aliyekuwa gavana wa Kisumu Jack Ranguma na waziri wa zamani Dalmas Otieno.

Wengine waliokuwa katika mkutano huo ni mbunge wa zamani wa Rangwe Martin Ogindo, aliyekuwa mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya simiti ya East Africa Portland na kampuni ya sukari ya Muhoroni Sugar Co Ltd, John Nyambok, mkuu wa biashara ndogondogo wa Benki ya KCB Christopher Migunde na mtaalamu wa masuala ya elimu Profesa David Otieno Okelo.

Mkutano huo uliandaliwa na Bw Owalo ambaye sasa ni mwandani wa Dkt Ruto baada ya kuachana na Bw Odinga.Dkt Ruto, hivi karibuni, alisema kuwa amekubaliana kufanya kazi na magavana zaidi ya 20 pamoja na mawaziri ambao hawajajitokeza hadharani kutokana na hofu ya kupoteza viti vyao.

Lakini mbunge wa Suba Kusini John Mbadi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kitaifa wa ODM, amepuuzilia mbali viongozi wa Nyanza waliokutana na ujumbe wa Dkt Ruto.

Bw Mbadi aliambia Taifa Jumapili kuwa viongozi hao waliokutana na ujumbe wa Dkt Ruto hana ushawishi wowote wa kisiasa katika eneo la Nyanza.Mbunge Maalumu wa ODM Rose Nyamunga pia amepuuzilia mbali viongozi hao akisema kuwa ‘wanatafuta pesa za kampeni kutoka kwa Naibu wa Rais’.

“Raila ndiye kiongozi wa pekee aliye na mamlaka ya kufanya mazungumzo na viongozi kutoka maeneo mengine ya nchi. Waliokutana na ujumbe wa Ruto wanapoteza wakati na wanasumbuliwa na njaa,” akadai Bi Nyamunga.

You can share this post!

KNUT: Walalama Sossion amesambaratisha chama

Hofu ya msambao mpya kanuniza kudhibiti corona zikipuuzwa