• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 8:03 AM
WALLAH: Usimtukane mamba kabla hujauvuka mto

WALLAH: Usimtukane mamba kabla hujauvuka mto

NA WALLAH BIN WALLAH

JUZI nilimsikia Mzee Shikaadabu akimkanya mjukuu wake aitwaye Kichwamraba akome kabisa ujeuri! Akamwambia, ‘Mjukuu wangu, ujeuri hujeruhi! Usiwe mjeuri wala usiwe mkaidi! Kumbuka mkaidi hafaidi hadi siku ya Idi!’

Nilijikuna kichwa nusura ning’oke nywele zote! Nikawaza kuhusu maafa ya mtu aliye mjeuri au mkaidi maishani! Nikajiambia kwamba, ‘Mkulima anapolima shambani, hupanda mbegu ziote!

Mimea ikishastawi avune mazao mazuri ayatumie kujikimu maishani! Lakini huyu mtu mjeuri au mkaidi, anapofanya ujeuri wake, anatarajia kupata faida au mavuno gani?

‘Baada ya kudadisi zaidi niliambiwa kwamba yule Kichwamraba mjukuu wa Mzee Shikaadabu alikuwa mjeuri mkosa adabu nyumbani kwa wazazi wake waliomlea, wanaomlisha na kumlipia karo ya masomo shuleni!

Licha ya hivyo, Kichwamraba aliupeleka ujeuri wake na ukaidi wake mpaka shuleni kwa walimu aliotarajia wangemsaidia kumfunza hadi afuzu apate elimu bora ya kumfaa kuja kuishi maisha mema duniani!!!

Tunapaswa kujua kwamba wazazi wana majukumu muhimu sana katika kuwalea na kuwatimizia watoto mahitaji yao maishani jinsi walivyo walimu shuleni!

Bila ya juhudi za walimu na kujitolea kwao kuwafunza na kuwaelekeza wanafunzi wao shuleni, amini usiamini, kufanikiwa kwa wanafunzi hao kungekuwa finyu sana!

Walimu ni nguzo muhimu sana masomoni!Kwa hakika mtoto akikorofishana na mzazi wake wakati ambapo hajafikia umri wa kujimudu kujitegemea maishani, ni msiba mkubwa sana!

Hata kama amefikia umri wa utu uzima lakini hana uwezo wa kujikimu mwenyewe maishani, atateseka tu! Mzazi aheshimiwe!!

Kule shuleni nako mtoto au mwanafunzi akimletea mwalimu wake ukorofi kabla hajasoma akahitimu elimu yake, anatarajia kupata nini?

Je, akitimuliwa kutoka shuleni au walimu wakisusia kumsaidia masomoni, atafanyaje baada ya kutelekezwa? Fikiri sana!!Ndugu wapenzi, hata kama unajua kuogelea mithili ya samaki, usimtukane mamba aliye majini kabla hujavuka mto!

Mamba ndiye mfalme mtoni! Mpe heshima zake ili uvuke uende ng’ambo salama salmini bila kung’atwa! Nawe mfanyakazi, usishindane na mkubwa wako kazini. Nyenyekea ufanye kazi upate ujira wako uishi uishie!

Tabia hii ya kumtukana mamba pia wanayo sana wanasiasa wakorofi wenye hulka za kumcharuracharura kiongozi wa nchi ambaye ndiye amirijeshi! Chonde chonde! Chuja kauli zako! Usimtukane mamba kabla hujauvuka mto! Usiseme hatukukwambia!!!!!

You can share this post!

PSG tayari kumsajili Ronaldo kucheza na Messi

FAUSTINE NGILA: Usilie ughali wa mafuta, nunua gari la...