Na KALUME KAZUNGU
WAKUU wa usalama Kaunti ya Lamu wanahofia ongezeko la idadi ya mifugo inayohamishiwa eneo hilo kutoka kaunti jirani za Tana River na Garissa tangu ukame ulipoanza kushuhudiwa humu nchini.
Kufikia sasa karibu mifugo 200,000 ikiwemo ng’ombe, mbuzi na kondoo tayari wamehamishiwa eneo hilo, hali ambayo imesababisha nyasi na maji kupungua.
Akizungumza na wanahabari muda mfupi baada ya kuandaa kikao cha dharura, Kamishna wa Kaunti ya Lamu, Irungu Macharia alisema ongezeko hilo la wafugaji limechangia mizozo kati ya wafugaji hao na wakulima wa sehemu tofauti tofauti za Lamu.
Alieleza haja ya mkutano wa dharura kuandaliwa kati ya viongozi wa Lamu na wale wa kaunti za Tana River na Garissa ili kujadili na kutoa suluhu kuhusiana na suala la wafugaji wa kuhamahama na ukame.