• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
HADITHI: Pengo asononekea hadhi ya chini wanayopewa walimu katika jamii

HADITHI: Pengo asononekea hadhi ya chini wanayopewa walimu katika jamii

NA SHIUNDU MUKENYA

VISA vya dharau kwa walimu vilimfanya Pengo awazie upya kuhusu taaluma yake. Alikumbuka jinsi viongozi kwingineko walivyolazimika au kulazimishwa kujiuzulu walipotoa kauli zilizoonekana kukidharau kikundi chochote katika jamii.

Lakini ilivyoonekana, mambo yalikuwa tofauti nchini Kavaluku. Viongozi wa kisiasa walitoa kauli za kuwadhalilisha walimu lakini hakuna lililofanywa zaidi ya kelele za mtandaoni zilizomithilishwa na vituko vya chura visivyomzuia ng’ombe kunywa maji.

Kelele za wananchi kuhusu viongozi waliowadharau walimu kwa kuwaita ‘watu wa vokali na watu wa kushika chaki tu’ zilififia na hatimaye zikatoweka.

Hakuna aliyerejelea kauli hizi. Pengo lakini hakuzisahau, alimkumbusha na kumlalamikia Sindwele kuhusu dharau hii.“Hilo si geni kwa walimu na haswa sisi wa shule za ulimwengu wa tatu, tumezoea dharau hizo. Umesahau msemo kuwa kizuri cha bwana Sweyyid kikiharibika ni cha mwalimu fundi.

Ni sisi mafundi wa kutupiwa vilivyoharibika na kupigiwa mifano ya watu duni katika jamii.” Kauli hii ya Sindwele japo iliuma, ilimkumbusha Pengo aliloambiwa na baba yake siku ile alipoipokea barua ya kuenda chuoni kusomea ualimu.“Una maana kuwa huko pia wanafundisha ualimu?”

Nzeki alimuuliza Pengo na kumjuza kuwa enzi zao watu ambao hawakuweza kuendelea na masomo ya chuo kikuu waliajiriwa kuwa walimu. “Kumbe mambo yamebadilika hivi?”

Mbali na mtazamo huu wa baba yake kuhusu ualimu, Pengo alikumbuka swali alilowahi kuulizwa na mwanafunzi wake mwanzoni kabisa mwa taaluma yake.

Wakati huo Pengo alikuwa barobaro aliyefundisha kwa nguvu zake zote na dhati ya moyo wake. Alipohitimisha kipindi, mmoja wa wanafunzi akaunyanyua mkono akaulize swali.

Mwanafunzi alianza kwa kumpongeza mwalimu kwa kipindi kizuri, “Lakini mwalimu mbona waonekana kuwa msomi hivi na hujawahi kupata kazi nzuri? Mbona ungali unang’ang’ania huu ualimu? Mbona usitafute kazi yenye staha kidogo?” mwanafunzi akauliza hatimaye.

Naam, haya yalitosha kumkumbusha Pengo stihizai walizopitia walimu.“Lakini mbona walimu hawa wasitumie kura zao kuwaadhibu hawa wanasiasa wenye jeuri?” akamuuliza Sindwele.

“Wewe wajua walimu walivyo watu wa kutafuta vijipeni vya ziada. Wao huajiriwa kusimamia uchaguzi na hivyo basi hawapigi kura. Isitoshe, kunayo ile dhana ya ‘mbaya wetu’ kama inavyosawiriwa katika tamthilia ya Ken Walibora. Kwamba kwa pamoja tunamchukia kiongozi yeyote anayetudhulumu, chuki hii hudumu tu hadi wakati wa uchaguzi kila mtu anaposimama na mwanasiasa wa kwao licha ya ubaya wa mwanasiasa huyo,” Sindwele akamfafanulia Pengo.

You can share this post!

LUGHA: ‘Maankuli’ au ‘mamkuli’ ni zao la kujifunza...

KAULI YA WALLAH: Ni busara kufikiri badala ya kupapia...