• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 1:15 PM
Pwani: Kiangazi chaleta maafa

Pwani: Kiangazi chaleta maafa

KALUME KAZUNGU na SIAGO CECE

KIANGAZI kimesababisha maafa katika kaunti mbalimbali za Pwani, ambapo watu wameauawa na wanyamapori huku mifugo ikiangamia.

Katika Kaunti ya Kwale, watoto wawili wa umri wa mwaka mmoja na miwili waliuawa na kuliwa na fisi wawili katika kijiji cha Baisa, tarafa ya Kinango.

Kisa hicho kilitokea Jumanne majira ya saa tatu unusu asubuhi, fisi hao walipovamia kijiji hicho ghafla.Watoto hao walikuwa wamelala ndani ya nyumba yao wakati mama akitekeleza shughuli za kawaida mita chache kutoka nyumbani humo.

Afisa Mkuu wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Kinango, Bw Fred Ombaka, alisema watoto hao hawangeweza kuokolewa kwa kuwa walijeruhiwa vibaya kichwani.

“Wanakijiji waliwawinda fisi hao na wakafaulu kumuua mmoja. Mwengine alitoroka,” akasema Bw Ombaka.Mama wa watoto hao Mulongo Tsimba alipiga kelele zilizovutia wanakijiji ambao walimkabili mmoja wa fisi hao.

Watu wanne walijeruhiwa kwenye makabiliano hayo.“Bi Mulongo ni miongoni mwa wale waliojeruhiwa. Ana majeraha ya kukwaruzwa mikononi, miguuni na usoni. Kalu Chiti na Mutuku Mutinda pia walijeruhiwa mikononi na miguuni na wamelazwa katika hospitali ya Samburu,” alieleza mkuu huyo wa polisi.

Chifu wa kata ndogo ya Chengoni, Bw Jackson Chengo, alisema fisi hao pia walikuwa awali wamevamia na kujeruhi watu wawili katika kijiji jirani.

Miili ya watoto hao wawili imelazwa kwenye hifadhi ya maiti ya hospitali ya Kinango.Wakazi wa Kinango, hasa wale wanaopakana na mbuga ya wanyama ya Tsavo, wamekuwa wakihangaishwa na wanyamapori wanaorandaranda mitaani wakitafuta maji na chakula msimu huu wa kiangazi.

Ukame pia umeathiri shughuli za masomo kwani wanafunzi hulazimika kufika shuleni kuchelewa, badala ya kurauka na kisha kuvamiwa na wanyama njiani.

Katika Kaunti ya Lamu, zaidi ya ng’ombe 500 tayari wamekufa katika maeneo ya Witu, Dide Waride, Chalaluma, Kitumbini,Nagelle, Pandanguo,Mavuno, Poromoko, Mkunumbi, Koreni, Mpeketoni, Hongwe, Bar’goni na Hindi.

Mkurugenzi wa Shirika la Kukabiliana na Ukame (NDMA) Kaunti ya Lamu, Bw Mohamed Dahir, alisema juma hili watazuru maeneo yote ya Lamu ambayo yanakumbwa na ukame ili kutathmini hali na kukusanya ripoti kamili.

Watu zaidi ya 100, 000 katika kaunti hiyo tayari wanakeketwa na makali ya baa la njaa pamoja na ukosefu wa maji hata ya kunywa.

Mwenyekiti wa Shirika la Mifugo na Masuala ya soko, Bw Kahlif Hirbae, aliiomba serikali kuzindua mpango wa kuwapa wafugaji lishe ya mifugo wao ili kuzuia wanyama hao wasiendelee kufariki kwa sababu ya makali ya ukame.

Bw Hirbae aliiomba serikali na wahisani kuwafidia wafugaji wote ambao wamepoteza mifugo kutokana na ukame ili wajiendeleze maishani.

“Tunahitaji msaada wa chakula cha ng’ombe. Inasikitisha kusikia taarifa kwamba mfugaji mmoja eneo kama vile Nagelle au Kitumbini amepoteza zaidi ya ng’ombe 100. Tunahitaji pia tufidiwe hasara hii,” akaeleza mwenyekiti huyo.

You can share this post!

Bei: Wakenya waishiwa pumzi

ODM yafanya uchaguzi wa wasimamizi tawi la Thika