• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:50 AM
TAHARIRI: Vijana wasikubali siasa za vurugu

TAHARIRI: Vijana wasikubali siasa za vurugu

KITENGO CHA UHARIRI

WAKAZI wa Kaunti za Siaya na Kisumu wanastahili pongezi kwa jinsi walivyoshughulikia ziara ya mfanyibiashara Jimmy Wanjigi.

Kwa kawaida mapokezi ya heshima kwa mtu ambaye ametangaza kuwa atampinga Kinara wa chama cha ODM Raila Odinga ndani ya chama chake, hayangefanyika.

Hili lilionekana Ijumaa katika Kaunti ya Migori, ambapo vijana walimrushia mawe Bw Wanjigi huku wakikatiza hotuba yake. Walisikika wakisema ‘Baba! Baba!’

Hiyo ilikuwa ishara kwamba eneo hilo ni ngome ya Bw Odinga pekee.

Kwa hivyo ni vizuri kwamba chama cha ODM kilikashifu kitendo hicho na kutaka Idara ya Polisi uchunguze waliokidhamini.

Tunaungana na ODM kumhimiza Inspekta Jenerali wa Polisi, Hillary Mutyambai aamuru uchunguzi. Watakapatikana na hatia ya kuwafadhili vijana kuzua vurugu hizo, washtakiwe.

Kenya ina sheria.

Katiba inatoa hakikisho kwamba kila Mkenya atakuwa na haki ya kushiriki katika kampeni na kuwaomba watu kura.

Kumzuia mtu au kumshambulia kwa mawe kwa sababu amepeleka kampeni zake eneo fulani, ni uhalifu.Ndio sababu viongozi wa Baraza la Wazee wa Luo kupitia mwenyekiti wake Mzee Willis Opiyo Otondi wanastahili pongezi.

Mzee Otondi alimkaribisha Bw Wanjigi Siaya, nyumbani wa Bw Odinga na akampa maneno ya kumtia moyo.

Aliamini kwamba Bw Wanjigi akiwa mwanachama wa maisha wa ODM, ana kila haki ya kuwania uteuzi wa chama hicho.Yeye si wa kwanza kufanya hivyo.

Manaibu vinara wa ODM Wycliffe Oparanya na Hassan Joho walifanya hivyo. Magavana hao wawili walilipa Sh1 miliono kila mmoja kwa chama cha ODM na kueleza azma zao za kutaka kuwania uteuzi wa kupeperusha bendera ya urais.

Ingawa Bw Joho wikendi alitangaza kujiondoa kwenye kinyang’anyiro, viongozi na wanachama wa ODM waliheshimu kujitokeza kwake kutaka ateuliwe.

Bw Wanjigi jana Jumapili pia alipata mapokezi mazuri jijini Kisumu, kitovu cha siasa za ODM.

Wakazi hao walitambua kuwa, Bw Odinga pia atataka kuomba kura katika maeneo yaliyo nje ya Nyanza. Kumvuruga Bw Wanjigi lingekuwa kosa kubwa kwa kiongozi mwenye hadhi ya kutaka kuwa urais wa Tano.

You can share this post!

Kenya Police warapua Vihiga kuingia FKF-PL

Wanjigi apata mapokezi mazuri Siaya baada ya kukataliwa...