• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
TAHARIRI: Ripoti ya Kemsa inakatisha tamaa

TAHARIRI: Ripoti ya Kemsa inakatisha tamaa

KITENGO CHA UHARIRI

KAMATI ya Bunge kuhusu Uwekezaji (PIC) iliyokuwa ikichunguza sakata ya wizi wa mabilioni ya fedha kupitia kandarasi zilizotolewa kiholela na Mamlaka ya Kusambaza Vifaa vya Tiba nchini (Kemsa), janga la corona lilipovamia Kenya mwaka 2020, haikufanya kazi ya kuridhisha.

Katika ripoti yake, kamati hiyo inayoongozwa na mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir, haikutoa mapendekezo ya kushtakiwa kwa baadhi ya wanasiasa wenye ushawishi serikalini waliotajwa wakati wa uchunguzi.

Sh7.8 bilioni zilitengwa na serikali kupambana na virusi vya corona lakini takribani Sh3.2 bilioni zinaaminika kuishia katika mifuko ya mabwanyenye wachache licha ya hospitali kukosa mitungi ya oksijeni na mavazi ya kukinga wahudumu wa afya dhidi ya virusi.

PIC ilipendekeza kampuni zilizopata kandarasi hizo zilizokuwa zikitolewa kiholela, zirejeshe fedha.

Wakati kamati hiyo ilipokuwa ikihoji wakurugenzi wa kampuni 102 zilizofanya biashara na Kemsa, walionufaika na kandarasi hiyo walikiri kukiuka sheria.

Wakenya walistaajabishwa kusikia baadhi ya wakurugenzi wa kampuni hizo wakidai kwamba waliomba Mungu kuwapa kandarasi.

Wengine walidai kwamba walikuwa wakipita karibu na jumba la Kemsa wakaitwa na kupewa kandarasi hiyo.Ukweli ni kwamba, ni vigumu kwa raia wa kawaida kupata kandarasi bila kuwa na ushawishi serikalini.

Kulikuwa na dalili kwamba kampuni hizo zilimilikiwa na watu wenye ushawishi serikalini waliojificha nyuma ya wakurugenzi hao.

Sakata hiyo ilipoibuka, Rais Uhuru Kenyatta, mnamo Agosti 2020, aliagiza Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kufanya uchunguzi na kuukamilisha ndani ya siku 21.

EACC ilikamilisha uchunguzi wake baada ya siku 21 kupita na kuwasilisha ripoti yake kwa Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Noordin Haji.

Bw Haji, hata hivyo, alikataa faili ya uchunguzi huo huku akiitaka EACC kufanya uchunguzi wa kina ili kupata ushahidi wa kutosha.EACC ilikuwa imependekeza kushtakiwa kwa wakurugenzi wa kampuni za f Accenture Kenya, Gadlab Supplies, Meraky Healthcare, Steplabs Technical Services, Wallabis Ventures, Shop n Buy na Kilig Ltd ambayo Naibu Mwenyekiti wa Jubilee David Murathe alikiri kuisimamia kuchukua mkopo katika Benki ya Equity.

Mbali na PIC, sakata hiyo imechunguzwa na Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Afya pamoja na Seneti.

Inaonekana sakata hiyo imeingia kwenye orodha ndefu ya visa vya ufisadi ambapo walipa ushuru wamepoteza mabilioni ya fedha bila wahusika kuchukuliw hatua.Idata ya Kuchunguza Uhalifu (DCI) haina budi kuingilia kati kuhakikisha kuwa fedha zote zilizopotea katika sakata hiyo zinarejeshwa na wahusika wanakamatwa.

You can share this post!

DINI: Unahitaji hekima kucheza karata zako vyema maishani...

Mbinu wanazotumia walaghai kuingiza bidhaa kutoka Somalia