• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Tumejifunza kutokana na makosa yetu ya zamani , KANU Fresh yasema

Tumejifunza kutokana na makosa yetu ya zamani , KANU Fresh yasema

Na CHARLES WASONGA

WAJUMBE wa chama cha Kanu wamemteua rasmi mwenyekiti wao Gideon Moi kuwania urais katika uchaguzi mkuu ujao.

Katika sherehe ya kufana iliyofanyika katika ukumbi wa Bomas of Kenya, Nairobi wajumbe hao vile vile walimtaka Seneta huyo wa Baringo kushirikiana na viongozi wengine wenye maono sawa ili kuboresha nafasi yake ya kushinda.

‘Kwa hivyo wajumbe wa Kanu wameafikiana kwa kauli moja kumteua Gideon Moi kuwa mgombeaji wa urais katika uchaguzi mkuu wa 2022,’ Katibu Mkuu wa Kanu Nick Salat akasema aliposoma maazimio ya wajumbe hao.

‘Gideon Moi amepewa idhini ya kushirikiana na viongozi wengine wenye maono sawa kwa ajili ya kuibuka mshindi katika uchaguzi huo,’ akaongeza huku akishangiliwa na zaidi ya wajumbe 3,000 waliohudhuria kongamano hilo.

Katika hotuba yake, Seneta Moi aliwashukuru wajumbe hao kwa kile alichotaja kama heshima kuu huku akiahidi kuzindua manifesto yake ‘hivi karibuni’.

‘Vile vile, ningependa kuwashukuru vinara wenzangu watatu katika muungano wa OKA na Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga kwa kuungana nasi leo kwa shughuli hii muhimu, akaongeza.

Vinara wa muungano huo wa One Kenya Alliance Kalonzo Musyoka (Wiper), Musalia Mudavadi (ANC) walikuwepo akiwemo kiongozi wa ODM Bw Raila Odinga.

Naye Kiongozi wa Ford Kenya Moses Wetang’ula aliwakilishwa na Mbunge wa Kiminini Chris Wamalwa kwani yuko katika ziara ya kikazi nchini Amerika.

Mabw Musyoka, Mudavadi na Odinga nao wamekuwa wakiuza sera zao kwa lengo la kutimiza ndoto zao za kuingia Ikulu 2022. ‘Leo (jana) ningependa kutangaza kuwa muda wa mapumziko umeisha. Tumerudi. Kuanzia sasa mambo yatakuwa tofauti; nawahakikishia, nawahakikishia,’ akasema Seneta Moi.

Alisema kwa kipindi cha miaka 20 ambapo Kanu imekuwa ikiunga mkono wagombeaji urais wengine, wamekuwa wakitafakari kuhusu yale yanapaswa kufanywa kwa njia tofauti kwa manufaa ya Kenya.

‘Tumejifunza kutokana na makosa yetu ya zamani na sasa tuko tayari kuipa Kenya uongozi bora. Ndani ya wiki moja ijayo nitatangaza mpango wangu wa namna ya kuboresha maisha ya Wakenya, haswa wanyonge,’ Seneta Moi akaeleza.

Alitaja ufisadi kama chanzo cha changamoto zinazowaathiri makundi mbalimbali ya Wakenya wakiwemo wafugaji, wakulima, wafanyabiashara na makundi ya vijana na akina mama.

‘Ni kutokana na azma yetu ya kukabiliana na kero hii ambapo chama chetu kimeibuka upya. Sisi ni Kanu Freshi’ Seneta huyo akasisitiza.

Katika hotuba yake awali, Bw Odinga aliwasilisha salamu za heri njema kutoka kwa Rais Uhuru Kenyatta huku akisifu Kanu na kukitaja kama chama ambacho kimefanya mengi mazuri nchini.

Hata hivyo, alisema kuwa kuna mambo kadha mabaya ambayo Kanu ilifanya na ambayo aliyataja kama ‘jambo la kawaida.

”Chama cha Kanu kimefanya mengi mazuri tangu kilipoanzishwa mnamo 1960s japo kuna mengine mabaya ambayo ni kawaida katika historia ya asasi yoyote,’ akasema huku akitoa historia Kanu tangu Kenya ilipopata uhuru hadi 2002 kilipoandolewa mamlakani.

Kwa upande wao Mbw Musyoka na Mudavadi pia walimsifia Seneta Moi wakimtaja kama kiongozi mwenye sifa hitajika kuwania urais.

‘Ndugu yangu Gideon ni mwanasiasa anayependa kusema ukweli. Sio mdanganyifu kama wanasiasa wengine. Tutatembea naye na ninawaomba nyie wafuasi wetu mtupe nafasi hiyo,’ akasema Bw Musyoka ambaye ni kiongozi wa Wiper.

Kongamano hilo pia lilihudhuriwa na wabunge kutoka vyama vya ODM, ANC na Jubilee wakiongozwa na kiongozi wa wengine katika bunge la kitaifa Amos Kimunya.

You can share this post!

Tumewafaa wateja wetu wakati wa corona – Safaricom

BENSON MATHEKA: TSC iwe na uwazi na usawa katika mpango wa...