• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 6:40 PM
Ajabu polo akimnyunyizia bawabu mkojo na kuacha kinyesi lojing’i baada ya kuporwa na kahaba

Ajabu polo akimnyunyizia bawabu mkojo na kuacha kinyesi lojing’i baada ya kuporwa na kahaba

NA MWANGI MUIRURI

Makutano, Embu

KULIZUKA kizazaa katika lojing’i ya mtaa huu baada ya polo kuamka na kupata kahaba aliyekuwa ameingia naye kupiga moyo pasi, amehepa na pesa na simu yake.

Kisa hicho cha saa nane usiku kilimgadhabisha jamaa huyo kiasi kwamba alimkojolea bawabu wa lojing’i hiyo akimlaumu kwa kushirikiana katika wizi huo.

“Wewe ndiye ulinikodisha chumba hiki. Uliniona nikiingia na mwanamke huyo na nikakuelezea vizuri kwamba tulikuwa tukeshe naye hapa. Mbona ukamkubalia atoke bila kunijulia hali?” akafoka.

Kalameni huyo aliyekuwa ameingia katika chumba hicho mwendo wa saa nne usiku akiwa mlevi, alisemekana kulemewa na usingizi wa pono na ndipo mrembo akaona atoke akaendelee kusaka wateja wa pesa zaidi.

Katika mabishano yaliyozuka kati ya polo na bawabu, iliishia sarakasi wakati jamaa alifungua long’i yake na kabla kieleweke, akamkojolea kwenye uso.

“Bawabu alikuwa tu amekaa kwa kiti chake katika malumbano hayo…Hakuna hatari iliyokuwa ikimwandama. Kuona polo hakuwa na mzaha, bawabu aliamka na akaanza kuhepa huku polo akimkimbiza kwa silaha hiyo ya mkonjo angani akimlenga,” akasema mdokezi.

Ilibidi wateja wengine wamshike kwa nguvu jombi huyo na wakamrejesha katika chumba chakem, ambapo pia alichafua matandiko ya kitanda pamoja na sakafu kwa mkojo na kinyesi kulipiza kisasi.

Aidha, polisi waliitwa asubuhi na polo akalazimishwa kuosha uchafu huo kisha akaachiliwa huru.

 

 

 

 

 

  • Tags

You can share this post!

Yaya aliyeangamiza afisa mkuu Kilifi alitoroshwa usiku kwa...

Seneta Nyutu aitaka Del Monte kukoma kuua vijana...

T L