• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 7:12 PM
Aliyejenga kijumba ndani ya nyumba kujificha akiona

Aliyejenga kijumba ndani ya nyumba kujificha akiona

NA RICHARD MUNGUTI

MSEMO kwamba mkono wa sheria ni mrefu ulitimia Aprili 6, 2023 polisi walipogudua pango alimokuwa anajificha mwanamke aliyetoroka asifungwe katika kesi mbili za ulaghai wa Sh4.9 milioni na ukwepaji kulipa ushuru wa Sh204 milioni.

Hata hivyo alipotolewa ndani ya pango na kufikishwa kortini Claire Marisiana Odimwa alifungwa miaka miwili gerezani kwa kosa la kumlaghai Bw Thomas Aul Ewald Sh4.9 milioni.

Alifungwa na hakimu mwandamizi Martha Nanzushi.

Alipopokea pesa hizo kutoka kwa Aul, mshtakiwa alimweleza alizitaka za kumpeleka jamaa wake ng’ambo kwa matibabu.

Polisi walimkuta Claire amejificha ndani ya kabati maalum aliyounda chini ya ngazi ndani ya nyumba mtaani Buruburu Nairobi.

Polisi aliyechunguza kesi zinazomkabili Claire alisimulia kortini vile walimkamata mshtakiwa.

“Mshtakiwa alikuwa na mazoea ya kuzima simu na kuifungua. Tulifuata masafa ya simu yake alipoipokea. Ilituelekeza hadi Buruburu,” Bi Nanzushi alielezwa.

Mahakama ilifahamishwa masafa ya simu yalitua katika makazi yake Buruburu lakini walipoingia ndani ya nyumba walimsaka hata katika dari na hawakumpata.

Lakini masafa ya simu yalionyesha angali hapo ndani ya nyumba.

“Tuliamua kuangalia ndani ya kabati iliyokuwa imefungwa katika panda ngazi hiyo. Salaalaa! Tulimpata ameketi mle ndani. Tulimkamata na kumpeleka kituo cha polisi,” afisa huyo wa polisi alisema.

Bi Nanzushi alifahamishwa na polisi kwamba “walimsaka Claire kwenye dari lakini hawakufanikiwa kumpata.”

Mshtakiwa alielezwa na hakimu kwamba alipokuwa hafiki kortini kesi ya ulaghai wa Sh4.9m ilisikizwa na kuamuliwa.

Mshtakiwa alihukumiwa kifungo cha miaka miwili ama alipe faini ya Sh300,000.

Claire alipelekwa tena mbele ya hakimu mwandamizi Bi Wandia Nyamu ambaye aliagiza apelekwe mbele ya hakimu Gilbert Shikwe anayesikiliza kesi ya kusababisha nchi ipoteze kodi ya Sh204 milioni.

Katika kesi hiyo Claire anadaiwa alipunguza uzito wa ngozi za ng’ombe zilizouzwa nje kati ya 2015 na 2016.

Alipunguza uzani wa ngozi hizo kwa kilo 3,862,264 zilizopelekea serikali kupoteza ushuru wa Sh204milioni.

Bi Wandia alikataa kumwachilia mshtakiwa kwa dhamana akimweleza dhamana ya zamani ilitwaliwa na serikali.

“Hakuna dhamana yoyote uko nayo. Ile ulipewa uliposhtakiwa ilitwaliwa na serikali ulipowacha kufika kortini,” Bi Nyamu alimweleza mshtakiwa.

Mshtakiwa aliagizwa afike mbele ya Bw Shikwe Aprili 14, 2023 kwa maagizo zaidi.

  • Tags

You can share this post!

Karua amkejeli Ruto kwa kuzindua mradi mara mbili

Mdogo wa Omanyala kuwakilisha Kenya riadha za Afrika za...

T L