NA PATRICK LANGAT
MAKAMISHNA wanne waasi wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) wanatarajiwa kukutana na wabunge Alhamisi, baada ya malalamishi manne kuwasilishwa yakishinikiza waondolewa afisini.
Makamishna hao ni Naibu Mwenyekiti wa tume hiyo, Juliana Cherera, Bw Francis Wanderi, Bw Justus Nyang’aya na Bi Irene Masit.
Makamishna hao wanne walikataa kuidhinisha matokeo ya urais wa Agosti 9, ambapo hatua yake ya mwisho huwa uthibitishaji.
Badala yake, walisema mchakato huo uliendeshwa kwa njia isiyo ya uwazi.
Ikiwa makamishna hao wanne wataondolewa katika tume hiyo, huenda Kenya ikapata tume mpya ya uchaguzi mwaka 2023, ikizingatiwa kuwa muda wa kuhudumu wa mwenyekiti wake, Bw Wafula Chebukati, makamishna Abdi Guliye na Boya Molu utakamilika Januari.
Tayari, mrengo wa Kenya Kwanza wake Rais William Ruto umezua utata, baada ya kuanzisha mpango wa kubadilisha wanachama wa jopo ambalo huwateua watu ambao huhojiwa kwa nafasi za makamishna katika tume hiyo.
Mrengo wa Azimio la Umoja-One Kenya, anaoongoza Raila Odinga, unapinga mswada ambao unapendekeza kupunguza idadi ya wanachama wa Tume ya Huduma za Bunge (PSC), ambayo huwateua wanachama wanne kati ya saba wa jopo hilo.
Mswada huo ambao umewasilishwa na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wa unapendekeza tume hiyo kuwateua wanachama wawili kutoka wanne, huku ikitenga nafasi zingine mbili kwa Kamati ya Kusimamia Mahusiano ya Vyama vya Kisiasa na Tume ya Utumishi wa Umma (PSC).
Chama cha Mawakili Kenya (LSK) na Baraza la Mashirika ya Dini (IRCK) zitadumisha nafasi zao za mwakilishi mmoja na wawili mtawalia, kwenye mageuzi mageuzi yaliyopendekezwa.
Malalamishi hayo manne yamewasilishwa na chama cha Republican Party, Kaasisi Dennis Ndwiga Nthumbi, Bw Geoffrey Lang’at na Bw Steve Gerry Owuor.
Wabunge katika Kamati ya Haki na Masuala ya Sheria (JLAC) watafanya kikao na walalamishi hao wanne kabla ya kupata majibu kutoka kwa makamishna hao.Kamati ya Bunge itawasilisha ripoti kuhusu ikiwa Bunge litamrai Rais William Ruto kubuni jopo maalum kutathmini ikiwa wanne hao wanafaa kuondolewa afisini au la.
Wabunge watapiga kura kuhusu ripoti itakayomuuliza Rais kubuni jopo itakayotathmini mienendo ya makamishna hao na kupendekeza ikiwa wanafaa kuendelea kuhudumu.
Hapo jana Jumatatu, Kiranja wa Wachache katika Bunge la Kitaifa Junet Mohamed, alipinga hatua ya kutaka makamishna hao kufika mbele ya wabunge, akisema utaratibu huo si halali.
“Hili halifai na ni jaribio la kukiuka Katiba na tararibu za Bunge. Kuondolewa kwa makamishna hakujadiliwi katika kamati ya JLAC,” akasema Bw Mohamed kupitia Twitter.
Subscribe our newsletter to stay updated