NA MASHIRIKA
JOHANNESBURG, AFRIKA KUSINI
MAHAKAMA Kuu ya Rufaa nchini Afrika Kusini jana Jumatatu ilisema rais wa zamani wa taifa hilo, Jacob Zuma, alipewa msamaha wa matibabu kutoka kwa kifungo cha gereza alichokuwa akitumikia mwaka 2021 kinyume cha sheria.
Hivyo, mahakama ilisema, kiongozi huyo anafaa kurejea gerezani kukamilisha kifungo chake.
Zuma, 80, alihukumiwa kifungo cha miezi 15 gerezani mnamo Juni 2021 kwa kukosa kufika mahakamani, hali iliyozua maandamano makali nchini humo.
Hata hivyo, kiongozi huyo alihudumu kwa miezi miwili pekee gerezani, ambapo baadaye alipewa msamaha wa matibabu katika hali tatanishi.
Msamaha huo ulitolewa na Mkuu wa Idara ya Magereza nchini humo, licha ya ushauri wa kamati ya matibabu ya idara hiyo kwamba Zuma hakuwa ametimiza masharti ya kupewa msamaha huo.
“Mahakama hii imeamua Zuma alipewa msamaha wa matibabu kinyume cha sheria,” ikasema mahakama ya rufaa kwenye uamuzi wake.
“Kisheria, Zuma hajamaliza kutumikia kifungo chake. Lazima arejee katika Kituo cha Kurekebishia Tabia cha Estcourt ili kukimaliza,” ikaeleza mahakama, ikirejelea gereza hilo, lililo kaskazini mashariki wa mji wa Durban.
Kulingana na tathmini za kimatibabu zilizorejelewa kwenye uamuzi wa mahakama, Zuma ana matatizo ya kiafya yanayohusishwa na mpigo wa juu wa damu, kiwango cha juu cha sukari katika damu yake na matatizo ya utumbo wake.
Zuma, ambaye alikuwa miongoni mwa watu walioukabili utawala wa ubaguzi wa rangi, alichaguliwa kama rais mnamo 2009.
Hata hivyo, alilazimika kuondoka uongozini 2018 kufuatia madai ya kushiriki katika sakata za ufisadi.
Licha ya tuhuma hizo, bado ana umaarufu mkubwa miongoni mwa wafuasi wa chama tawala cha African National Congress (ANC), wengi wakimwona kama mtetezi wa watu maskini na wanaonyanyaswa.
Wakati kifungo chake cha gereza kilipotangazwa, maandamano makali yalizuka katika maeneo tofauti nchini humo, hali iliyosababisha vifo vya watu 350. Maduka kadhaa pia yaliporwa.
Huenda agizo hilo la Mahakama Kuu ya Rufaa likakosa kuwa la mwisho kumhusu Zuma, kwani bado ana nafasi ya kwenda katika Mahakama ya Kikatiba, kwani ndiyo ya juu zaidi nchini humo.
Mwezi uliopita – Oktoba – wasimamizi wakuu wa magereza walitangaza kuwa kifungo cha miezi 15 alichohukumiwa Zuma kimekamilika.
Tangu wakati huo, amehudhuria mikutano kadhaa ya umma, huku akiimba na kucheza densi mbele ya wafuasi wake.
Pia, amekuwa akimkosoa vikali mrithi wake, Cyril Ramaphosa, kwa madai ya ufisadi na uhaini.
Ramaphosa atashiriki kwenye kongamano muhimu la ANC mwezi ujao Desemba ambapo anatafuta uungwaji mkono wa chama kumwidhinisha kuwania urais kwa muhula wa pili.
Hili ni licha ya tuhuma za ufisadi zinazomkabili, kwani anadaiwa kuficha mamilioni ya pesa nyumbani kwake.
Subscribe our newsletter to stay updated