• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 5:50 AM
CHARLES WASONGA: Walimu wakuu wanaoendelea kutoza ada za ziada waadhibiwe

CHARLES WASONGA: Walimu wakuu wanaoendelea kutoza ada za ziada waadhibiwe

Na CHARLES WASONGA

NIMEWAHI kuandika mara si moja katika safu hii kwamba ni haki ya kila mtoto nchini kupata angalau elimu ya msingi. Elimu hii inaaza kutoka kiwango cha chekechea hadi kile cha shule ya upili.

Kwa hivyo, kuwa mujibu wa kipengele cha 43 (f) cha Katiba ya sasa, ni wajibu wa serikali kuhakikisha kuwa watoto wote wanapata haki hii.

Hii ndio maana serikali imeanzisha, na inafadhili, sera mbalimbali katika sekta ya elimu kama vile elimu bila malipo katika shule za msingi na kupunguzwa kwa gharama ya elimu katika shule za upili.

Isitoshe, serikali inatekeleza sera ambapo wanafunzi wote waliofanya mitihani wa kitaifa wa darasa la nane (KCPE) wanapata nafasi ya kujiunga na shule za upili bila kuwekewa vizingiti kama alama duni au ukosefu wa karo.

Muhimu zaidi ni kwamba serikali imeweka viwango vya karo ambavyo vinapaswa kutozwa wanafunzi katika viwango mbalimbali vya shule za upili, ili kukinga wazazi dhidi ya kupunjwa na walimu wakuu walaghai.

Kwa hivyo, ningependa kumhimiza Waziri wa Elimu George Magoha kuwachukulia hatua kali zaidi walimu wakuu wanaokiuka mwongozo wa karo uliotangazwa na wizara yake mapema mwezi jana.

Kulingana na mwongozo huo wazazi ambao watoto wao wanasomea shule za upili za kitaifa watalipa Sh45,000 kwa mwaka na wale ambao watoto wao wanasomea shule za upili ngazi za kaunti na kaunti ndogo wanapaswa kulipa Sh35,000 katika mwaka ujao wa masomo.

Hii ni kwa sababu muhula ujao umepunguzwa kutoka wiki 39 hadi 30 kutokana na janga la Covid-19.Lakini kuna walimu wengine wakuu ambao tayari wameanza kukiuka mwongozo huu kwa kutoza ada zaidi haswa kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza watakaoripoti shuleni kuanzia Agosti 2, 2021.

Wanatoza kati ya Sh5,000 na Sh35, 000 kama ada ya kufadhili ujenzi wa miundo msingi, bila idhini ya wizara ya elimu inavyohitaji kisheria.

Haitoshi kwa Katibu wa Wizara ya Elimu Dkt Julius Jwan kuwaonya walimu wakuu kama hawa au kuwashauri wazazi kutolipa ada hizo, bali awasimamishe kazi, kwa muda, walimu wakuu kama hawa ili iwe funzo kwa wengine wenye nia ya kushiriki uovu kama huo.

Isitoshe, walimu wakuu kama hawa wanafaa kushtakiwa kwa ukiukaji wa Katiba kwani kitendo hicho cha kuwatoza wanafunzi ada hizo za ziada kinahujumu haki ya wanafunzi, hususan kutoka jamii masikini kupata elimu, kulingana na kipengele cha 43 cha Katiba.

Aidha, kinaathiri sera ya serikali ya kuhakikisha kila mwanafunzi anajiunga na shule ya msingi.

You can share this post!

Jumwa akwamilia UDA, adai Ruto ataingia Ikulu 2022

Kibarua kwa Samboja kiti chake kikimezewa mate