SHANGAZI;
Kabla tuanze uhusiano, mpenzi wangu alinionya kuwa hawezi kuishi na mwanamume asiyemtosheleza chumbani. Nimeanguka mtihani huo na ameamua kuniacha. Nifanyeje?
Hatua ya mwanamke huyo ya kukuonya mapema ilikusudiwa kukuandaa kuhusu jinsi ya kudumisha uhusiano wenu. Kama umeshindwa huwezi kumlaumu kwa sababu hayo ndiyo maumbile yake.
Mke wangu ameniambia jirani yetu anamtaka. Amemhangaisha sana kimapenzi na ndio maana ameamua kuniambia ili nimkomeshe. Nimeshangaa sana kwa sababu huyo pia ni rafiki yangu. Nishauri.
Huyo si rafiki tena bali ni adui mkubwa. Ameamua kuweka kando urafiki wenu kwa sababu ya tamaa. Mke wako amethibitisha uaminifu wake mwako. Usikubali aendelee kuhangaishwa.
Nimekuwa na mke kwa miaka miwili na tumejaliwa mtoto mmoja. Juzi mama yake alikuja kwetu na mtoto mwingine. Kumbe mke wangu alizaa na mpenzi wa awali! Nifanye nini?
Mke wako alihofia ukijua ukweli huo utamuacha. Kuna usemi kwamba kosa moja haliachi mke. Isitoshe, mtoto ni baraka. Kama unampenda, msamehe na umkubali mtoto huyo kuwa wako.
Nimeamua kuolewa na mwanamume chaguo la moyo wangu. Nampenda sana na sitaki kumpoteza kwa wanawake wanyakuzi wa waume wa wenyewe. Nafikiria kumpumbaza kwa dawa. Waonaje?
Kama unazungumzia kuhusu mitishamba, mimi kamwe sitambui wala siamini ushirikina. Mpenzi wako hawezi kulazimishwa kufanya chochote. Kama si mwaminifu kwako atanyakuliwa tu.