SHANGAZI;
Mpenzi wangu anafanya biashara ya pombe. Baadhi ya wanaume wateja wake wanamtaka kimapenzi lakini amenihakikishia kuwa ananipenda na hawezi kupenda mwingine. Waonaje?
Ni kawaida kwa wanaume kutongoza wanawake katika maskani za pombe. Tabia hiyo huchochewa zaidi na ulevi. Mpenzi wako amekuchagua wewe na amekuhakikishia kuwa hataki mwingine. Ondoa shaka.
Kuna mwanamume ambaye ananitaka kwa lengo la kunioa. Ameniambia alikuwa na mke lakini wakaachana. Nampenda lakini nina wasiwasi huenda mkewe akaamua kurudi. Nishauri.
Hali kwamba mwanamume huyo amekwambia kuhusu ndoa yake ya awali ni ishara kuwa anakupenda. Muulize walivyoachana na iwapo kuna matumaini ya kurudiana. Ukitosheka na majibu yake, kubali ombi lake.
Nina mchumba ambaye nataka kumuoa. Ametimiza mambo yote ambayo mwanamume anahitaji kwa mwanamke isipokuwa moja tu. Hajui kupika! Nifanyeje?
Ujuzi hutokana na mafunzo. Mambo yote tunayojua tumejifunza shuleni na katika jamii tunamoishi. Kuna vyuo vingi vya mafunzo ya upishi ambako anaweza kupokea mafunzo. Shauriana naye.
Nina miaka 32. Kuna mwanamume anayetaka tuwe wapenzi. Nina hisia kwake lakini nimemwambia anipe muda nifikirie. Sasa nimegundua anamtaka mwanamke mwingine. Nifanyeje?
Shughuli ya kutafuta mpenzi ni jambo la kubahatisha. Mwanamume huyo hajui kama utakubali ombi lake na ndiyo maana anajaribu kwingine ili akikosa huku apate kule. Kama unampenda mwambie kabla hajapata mwingine.