Na MWANDISHI WETU
Kwa wengi usafi ni mojawapo ya mambo muhimu yanayozingatiwa katika mahusiano.Kwa upande wa wanawake, wanapomsaka mpenzi, mchumba au mume, usafi wa mwili, mavazi na hata tabia huongeza alama kwa kaka anayenuia kuvutia macho yao.
Lakini sio wote walio na msimamo unaoakisi kauli hii. Mfano mzuri ni Jenah. Ni mkaguzi wa mahesabu katika shirika moja la kimataifa lenye makao yake jijini Nairobi.Binti huyu mwenye umri wa miaka 36 bila shaka ana kisomo ajira ya kutamaniwa mbali na kuwa na mfuko mzito kifedha.
Kutokana na ajira yake ya haiba ya juu, Jenah hukutana na baadhi ya watu mashuhuri na wenye mamlaka, mbali na kusafiri kwenda ng’ambo mara kwa mara.Ni suala ambalo litakufanya utarajie kuwa inapowadia katika masuala ya mahaba, basi ana jicho kali la kutafuta madume watanashati, wenye kisomo na taaluma za hali ya juu.Iwapo hayo ni mawazo yako, basi umekosea kwani Jenah ambaye bado anasaka mume wa kumuoa, ana jicho tofauti anapowinda dume lake.
Kwanza kabisa huku wanawake wengi wakifurahishwa na akina kaka wanaojua kujishughulikia kimwili na kuzingatia usafi, binti huyu anapagawishwa na madume wanaofurahia uchafu, kama anavyosimulia.
“Nikisema madume wanaofurahia uchafu namaanisha akina kaka wasiooga, wasiosugua meno, wenye makwapa yanayovunda, wasiochana nywele wala kubadilisha suruali zao za ndani. Sitaki kaka anayejipaka mafuta.
Ili uwe mpenzi wangu lazima uwe tayari kupuuza mwonekano wako kabisa. Sipendi mwanamume aliyenyoa nywele wala kushughulikia ndevu zake. Sivutiwi na mwanamume anayenyoa nywele katika sehemu yoyote mwilini. Sifurahii mwanamume anayekata kucha wala anayebadilisha mavazi yake. Sivutiwi na kaka anayejipulizia marashi, badala yake nafurahia uvundo wa jasho.
Napenda nikumbane na uvundo kutoka kila sehemu, kila mpenzi wangu anaponisongea. Kwangu, hiyo ni ishara ya ushari na dalili maalum ya jinsia ya kiume. Kwangu mwanamume anayezingatia sana usafi na mwonekano wake, ni sawa na binti.
Kitabia, pia kaka huyu asionyeshe ustaarabu. Kwa mfano kama ni kula, basi asiogope kuwa mlafi. Anapotembea, anajamba mbele ya watu bila aibu au kujificha. Anachakura pua na kuchokonoa meno kinywa kikiwa wazi na tena mbele ya watu, mezani.Kwangu usafi na ustaarabu wa mwanamume unaoondoa sifa za kiume.
Naamini kwamba mwanamume anapoonyesha usafi na adabu, basi kuna uwezekano mkubwa kwamba ni dhaifu, hasa katika masuala ya chumbani.Kuna baadhi ya watu wanaonichukulia kuwa wazimu wanaposikia kuhusu vigezo vyangu vya kusaka mpenzi. Lakini sitishiki kwani kipendacho moyo hula nyama bichi, na kwangu hizo sifa ndizo nizipendazo”.