NA MERCY KOSKEI
FAMILIA ya mwanamume aliyeuwawa katika eneo la Stima line, Kaunti ya Nakuru Jumatano Julai 19, 2023 wakati wa maandamano kushinikiza serikali kushusha gharama ya maisha inataka haki na waliohusika kukamatwa.
Benjamin Indi, 32, mwendesha bodaboda anadaiwa kupigwa risasi na polisi wakati wa makabiliano kati ya waandamanaji na maafisa wa polisi.
Kulingana na ndugu ya marehemu Bw Christopher Heman, kabla ya kuuwawa Indi aliondoka nyumbani na kuelekea katika steji ya bodaboda ambapo alikuwa akiendeshea shughuli zake kwa miaka mitatu, mita chache kutoka alikofariki.
Hata hivyo, saa chache baadaye alipokea simu ya huzuni kutoka kwa jirani yake akimjulisha kuwa kaka yake ameuawa kwa kupigwa risasi na kuwa anatakiwa kufika eneo la tukio.
Jambo hilo lilimfanya kuwapigia marafiki na wafanyakazi wenzake simu ambapo walimthibitishia kuwa Bw Indi alipigwa risasi.
Hata hivyo, alipowasili tayari ulikuwa umeondolewa na maafisa wa polisi na kupelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Nakuru City.
Kulingana na Bw Hemman, kakake alipata jeraha la risasi kwenye jicho lake la kulia.
Bw Heman alieleza Taifa Leo Dijitali kuwa kwa sasa wametembelea afisi ya chifu ili kupewa kibali cha kuanzisha mipango ya mazishi.
“Sina uhakika alikuwa miongoni mwa waandamanaji, alikuwa akifanya kazi eneo hilo. Huenda alikuwa hapo au alinaswa katika mapigano kati ya polisi na waandamanaji. Sababu za kupigwa risasi zingali kitendawili kwetu na tunachotaka kama familia ni haki,” alisema.
Alimkumbuka marehemu kuwa kijana mchapakazi ambaye siku zote alijitahidi kutunza familia yake licha ya kutengana na mkewe miaka miwili iliyopita.
Bi Elizabeth Andami, dadake, alikubuka mara ya mwisho kuwa na nduguye akisema kuwa alifika nyumbani kwake eneo la Pondamali siku ya Jumapili.
Alisema kuwa walikula chakula cha jioni pamoja kabla ya kuondoka huku akiahidi kwamba angerejea Jumanne jioni.
Hata hivyo, siku ya Jumanne Imbi alimpigia simu na kumwarifu kuwa ameshikika kazini na kuwa atafika siku ya Jumatano jambo ambalo halikufanyika.
“Wanataka tufanye uchunguzi wa maiti na tunajua sababu ya kifo chake. Hatuna pesa za kumwaga, badala yake tunataka kuzitumia kwa gharama ya mazishi. Sisi ni yatima, hatuna mtu wa kumtegemea,” alisema huku akitokwa na machozi.
Familia hiyo kwa sasa inaomba wasamaria wema kuwasaidia kusafirisha mwili nyumbani kwao Kaunti ya Siaya kwa minajili ya mazishi.