NA TITUS OMINDE
MAHAKAMA ya Kitale imeagiza aliyekuwa Gavana wa Trans Nzoia Patrick Khaemba kumlipa mwanamke raia wa Uganda Sh236,000 kila mwezi za kumtunza mtoto.
Hii inafuatia ombi la mwanamke huyo katika kesi aliyomshtaki gavana huyo wa zamani akitaka awe akimtunza mtoto huyo.
Mwanamke huyo anamlaumu Bw Khaemba kwa kukosa kumpa pesa hizo za kutunza mtoto kwa zaidi ya miaka kumi.
Stakabadhi za kesi zinaonyesha kuwa mwanamke huyo alizaa mtoto huyo na Bw Khaemba mwaka wa 2013.
Aliambia Mahakama kwamba Bw Khaemba alitelekeza majukumu yake kama baba na akamuacha ang’ang’ane kulea mtoto peke yake.
Katika hati ya kiapo kupitia wakili wake John Bororio, aliambia mahakama kwamba Bw Khaemba hajakuwa akimpa pesa za kutunza mtoto tangu 2013.
Korti ya kutatua kesi za watoto imeagiza Bw Khaemba kuanza kulipa Sh236,000 kila mwezi za kumtunza na pia kushughulikia mahitaji ya matibabu ya mtoto huyo. Agizo hilo litaanza kutekelezwa mara moja.
“Mshtakiwa ameagizwa kutoa pesa za huduma za matibabu au bima ya afya ya mtoto huyo kesi ikiendelea kusikilizwa hadi itakapoamuliwa,” hakimu alisema.
Subscribe our newsletter to stay updated