VIONGOZI jana waliendelea kutoa hisia mseto kuhusu hatua ya wabunge watano wa mrengo wa Kieleweke kuhamia mrengo wa Tangatanga unaoongozwa na Naibu Rais William Ruto.
Gavana wa Machakos Alfred Mutua alipuuzilia mbali hatua hiyo akisema haikutokani na kuimarika kwa umaarufu wa mrengo huo mashinani na kudorora kwa umaarufu wa Rais Uhuru Kenyatta.Alidai wabunge Gathoni Wa Muchomba (Mbunge Mwakilishi wa Kiambu), Gabriel Kago (Githunguri), Samuel Gachobe (Subukia), Simon Kingara (Ruiru) na David Gikaria (Nakuru Mjini Mashariki) waliongozwa na masilahi yao kibinafsi wala sio ule wa raia wanaowawakilisha.
“Hawa ni watu waliohongwa kuhamia mrengo wa Tangatanga wakisingizia kutimiza matakwa ya wapiga kura katika maeneo bunge yao,” akasema Gavana huyo katika mahojiano katika runinga ya Citizen Alhamisi asubuhi.
Hata hivyo, Dkt Mutua hakutoa ushahidi wa kuthibitisha madai yake ambayo yalikashifiwa vikali na Seneta wa Nandi Samson Cherargei ambaye pia alikuwa akishiriki katika kipindi hicho cha mahojiano kuhusu masuala ibuka katika ulingo wa siasa.
“Madai kama haya ambayo yametolewa na Gavana Mutua hayana msingi wowote. Ni madai ya uwongo. Wabunge hao na wengine wanaohamia mrengo wa Tangatanga kutokana na sera zake zinazotetea masilahi ya wananchi wa kawaida.
Kimsingi, wabunge hao wanajiunga na mrengo ambao utashinda katika uchaguzi mkuu ujao,” akasema Bw Cherargei.Bi Wamuchomba na wenzake, walisema walihamia mrengo Tangatanga kutii mwelekeo wa kisiasa katika maeneo bunge yao na ukanda wa Mlima Kenya kwa ujumla.
Hata hivyo, Dkt Mutua alishauri kuwa vyama au miungano ya kisiasa nchini inapaswa kuundwa kwa misingi ya sera na itikadi maalum wala sio kwa nia ya kushinda katika chaguzi kuu.“Tunafaa kuimarisha siasa zetu ili vyama au miungano tunayobuni iwe ni yenye sera na itikadi maalum.
Hii ndio njia ya kipekee ikatayozuia tabia mbaya ya wanasiasa kuruka kutoka chama kimoja hadi nyingi au muungano mmoja hadi mwingine wakidhani kuwa vyama hivyo ni maarufu,” akasema Gavana huyo wa Machakos.
Kwa upande wake Seneta wa Kiambu Kimani Wamatangi aliwakosoa wabunge hao waliochaguliwa na tiketi ya chama cha Jubilee lakini sasa wanajinasibisha na chama kipya cha United Democratic Alliance (UDA).Bw Wamatangi ambaye ndiye kiranja wa wengi katika Seneti alisema kuwa wabunge hao wanawakosea wapiga kura waliowachagua kwa matarajio kwamba wangetekeleza manifesto ya Jubilee kwa kipindi cha miaka mitano.
“Wananchi waliowachagua wabunge hawa ambao sasa wanahamia UDA au mirengo mingine wanafaa kuwauliza ikiwa wametimiza ajenda na manifesto ya Jubilee au la. Ikiwa hawajafanya hivyo basi wanasiasa kama hawa wanafaa kukataliwa katika uchaguzi mkuu ujao,” akaeleza.
Bw Wamatangi aliongeza kuwa kuhama kwa wabunge hao ni kwa “maneno tu” wala hakutambuliwi kisheria.“Kama kweli wamehama, wangejiuzulu nyadhifa zao na kurejea kwa wananchi kuomba wachaguliwe kwa tiketi za vyama vipya,”alisema.
Bila kufanya hivyo, huko kuhama kwamba kutachukuliwa kama hatua isiyo na maana yoyote,” akaeleza.Alipoulizwa ikiwa iwapo Bw Wamuchomba na wenzake wataadhibiwa na chama cha Jubilee kwa kuamua kuiasi na kuendeleza sera za mrengo mwingine wa kisiasa, Bw Wamatangi alisema hawezi kujibu swali hilo “kwa sababu mimi sio kiongozi wa Jubilee”.
“Mimi sio kiongozi wa Jubilee wala mtu aliyetwikwa wajibu wa kuhakikisha sheria inafuatwa. Lakini Sheria ya Vyama vya Kisiasa inasema wazi kwamba ikiwa utaunga mkono chama kingine cha kisiasa kando na kile ulichokitumia kuingia uongozini, unapaswa kujiuzulu na kuomba idhini nyingine kutoka kwa wapiga kura,” akasema Bw Wamatangi.
Hata hivyo, Mbunge wa Bahati Kimani Ngunjiri ambaye ni mwenyekiti wa Kundi la Wabunge kutoka kaunti ya Nakuru jana alichangamkia hatua ya wabunge hao akisema hii ina maana kuwa falsafa ya vuguvugu la “Hustler Nation” imekubaliwa na wananchi.
“Viongozi hawa wanachukua hatua hiyo kulingana na matakwa ya wananchi. Wakenya wanataka sera ya kiuchumi inayoanza mashinani kwenda juu. Hii ndio injili yetu kama wakereketwa wa “Hustler Nation” akasema.