Na OSCAR KAKAI
WASIWASI umeibuka kuhusu wazazi na wakazi wa miji mikubwa katika kaunti ya Pokot Magharibi wanaopoteza pesa wakishiriki kamari.
Baraza la Wazee wa Jamii ya Wapokot wanasema kwamba michezo mingi ya kamari imeibuka katika kaunti hiyo na watu wengi wamekuwa masikini kwa kuishiriki.
Mwenyekiti wa baraza hilo John Muok alionya wakazi dhidi ya kushiriki michezo hiyo akisema ni hatari kwa maisha yao.
“Watu wanauza mifugo yao kwa wingi na kuweka pesa katika kamari bila kujua kwamba ni mchezo wa pata potea. Wengi wao hawajui kwamba katika kamari, sio lazima mtu ashinde. Mtu hushinda kwa bahati tu,” alisema akiwa Kapenguria.
Haya yalijiri wiki moja baada ya kufichuliwa kuwa Wakenya walio na umri wa miaka 55 na zaidi wanaongoza kwa uchezaji kamari nchini.