NA MERCY KOSKEI
MAAFISA wa polisi katika katika Kaunti Ndogo ya Narok Kaskazini wanachunguza kisa ambapo mwanamume mwenye umri wa miaka 62 anadaiwa kumuua mwanawe wa miaka 12.
Kisa hicho cha Septemba 22, 2023 kilitokea katika kijiji cha Kipendeni, Wadi ya Olposimoru, na kufuatia kutiwa mbaroni kwa mwanamume huyo.
Inasemekana aliangamiza mwanawe kwa kumkatakata kwa panga kichwani.
Kulingana na ripoti ya polisi, mshukiwa kwa jina Samuel Landichi alimuua mtoto wake wa kiume katika boma lake kwa sababu zisizojulikana.
Kisa hicho kiliripotiwa na naibu chifu wa Olengape, Douglas Sadera, ambapo alielekeza maafisa kutoka Idara ya Uchunguzi wa Jinai na Uhalifu (DCI) katika eneo la mkasa kuanzisha uchunguzi kubaini kiini cha mauaji hayo.
Mwili wa mtoto huyo umepelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha hospitali ya kaunti ndogo ya Olenguruoni, ukisubiri kufanyiwa upasuaji.
Wakati huo huo, Landichi anazuiliwa katika Kituo cha Polisi cha Olokurto huku akisubiri kufunguliwa mashtaka ya mauaji mnamo Jumatatu, Septemba 25, 2023.