NA STEVE OTIENO
TUME ya Kitaifa ya Haki za Binadamu (KNCHR) imewaonya maafisa wa polisi na vyombo vya dola dhidi ya kutumia nguvu kupita kiasi ikiwemo kuwatesa raia, kuwanyima haki waliokamatwa wakiandamana kupinga sera za serikali na kuwanyima dhamana.
Aidha KNCHR inasema ni ukiukaji mkubwa wa Katiba kwa polisi na maafisa kufanya misako kwa unyama wa hali ya juu na hata kuidharau mahakama kwa kuwafurusha wanahabari wakifuatilia baadhi ya kesi za viongozi wa Azimio La Umoja-One Kenya.
“Tayari maafisa wanadaiwa kuwateka nyara watetezi wa haki za binadamu na kuwajeruhi raia wasiokuwa na hatia,” amesema mwenyekiti wa KNCHR Roselyne Odede akihutubu jijini Nairobi leo Jumanne.
KNCHR inataka uchunguzi uanzishwe kuwatia hatiani waliowatesa raia na kutekeleza uhalifu mwingine dhidi ya binadamu.
Pia tume hiyo inataka mahakama ziheshimiwe, uchunguzi wa kina ufanywe ili maafisa wanaojifanya wanahabari huku wakihangaisha raia wamulikwe na wachukuliwe hatua kali.
Muhimu zaidi KNCHR inataka haki za makundi spesheli katika jamii na raia wenye changamoto mbalimbali wachungwe.