• Nairobi
  • Last Updated May 1st, 2024 3:13 PM
Kustawisha afya za watu ndio chanzo cha kujenga taifa lililo bora

Kustawisha afya za watu ndio chanzo cha kujenga taifa lililo bora

NA MASHIRIKA

Hakuna kitu chenye thamani duniani kama mtu kuwa na afya bora. Afya bora ndio inampa mtu nguvu ya kuweza kufanya shughuli zake mbalimbali ikiwemo kujitafutia riziki kwa ajili ya kujikimu kimaisha. Ni kama msemo wa Kiswahili unavyosema “Bora Afya Kuliko Mali”, yaani ukiwa na mali huku afya yako imezorota inakuwa haina faida yoyote.

Hivi sasa China imefanya maamuzi makubwa na kuweka malengo ya kuzidi kuijenga jamii ya China yenye afya bora, ambapo mwaka 2016 ilitoa waraka wa “China yenye Afya 2030” ili kutangaza mpango wa utekelezaji mnamo Julai mwaka huu, kwa ajili ya kutekeleza mpango wa Afya nchini kutoka 2019 hadi 2030. Zaidi ya hayo, kuna mwelekeo wa kutatua shida za upatikanaji wa huduma za afya na kujitahidi kuhakikisha zinawafikia watu.

Rais Xi Jinping aliwahi kusema kwamba “Haiwezekani watu wote kuwa na ustawi bila ya watu wote kuwa na afya”. Kwa hiyo maneno haya moja kwa moja yanahimiza mamlaka husika kuwekeza na kuweka kipaumbele kwenye kuboresha huduma za afya kuanzia ngazi ya mashinani, kuhimiza upatikanaji sawa wa huduma za umma za msingi mijini na vijijini na kuwapatia watu huduma rahisi, salama, zenye ufanisi na watakazomudu za afya.

Tukichukulia mfano wa kisiwa kidogo cha Shiye, cha China, kilichozungukwa na maji ya mto Yangtze ambacho ni vigumu kukifikia, zamani wakazi wake sio tu walikuwa na hofu ya kuugua bali waliogopa hata kusafiri nje ya kisiwa hicho kwasababu ya mawasiliano duni na nje ya kisiwa. Lakini mabadiliko makubwa yanaonekana sasa, baada ya rais Xi kufanya ziara ya ukaguzi mwaka 2014 kwenye mji huo. Hivi sasa, watu hawana haja tena ya kuondoka kwenda nje ya kisiwa kutafuta matibabu hata kwa magonjwa madogo.

Katika miaka kadhaa iliyopita vimeshuhudiwa vitengo vitano, vikiwemo vya magonjwa ya moyo na kisukari vikianzishwa kwa ushirikiano wa pamoja na Zahanati ya Mji wa Shiye na Hospitali za Huduma za Afya za mji wa Zhenjiang. Zahanati hiyo sasa ina vifaa vya kisasa vya kupimia magonjwa kwenye kila kitengo, huku watu wake wakifurahia huduma za matibabu zinazotolewa na hospitali za mji huo.

Huu ni mfano mmoja tu kwa hapa China, mabadiliko mengi yameshuhudiwa baada ya rais mwenyewe kufanya ziara za ukaguzi kwenye maeneo mbalimbali ya nchi, na hii ni kutokana na azma yake ya kutaka kuifanya jamii ya China iondokane na magonjwa ambayo yanasababisha umasikini, kwani anaamini kushughulikia umasikini unaosababishwa na magonjwa na kutokea tena kwa umasikini kwasababu ya magonjwa ndio njia ya kujinasua, na hili ndio lengo lake kuu kabisa.

Jamii ikiwa na afya njema, watu wake wanakuwa na maisha mazuri na marefu, hivi sasa hapa China wastani wa watu kuishi ni miaka 76 hadi 77. Hii inatokana na juhudi na kampeni mbalimbali za kuhamasisha umma kutilia mkazo na umuhimu afya bora.

Katika nchi za Afrika suala la afya limekuwa na changamoto kubwa sana. Ingawa serikali nyingi zinajitahidi kutoa kipaumbele katika huduma za afya zenye ubora na zinazowafikia wananchi wote, lakini bado inaonekana kana kwamba haitoshi. Maendeleo ya nchi yoyote ile yanaletwa na wananchi wenye afya na wenye uwezo wa kuzalisha mali. Hivyo serikali zinapaswa kuiangalia kwa jicho pevu sekta ya afya.

Hivi sasa dunia inakabiliwa na janga la COVID-19, janga hili limefichua udhaifu wa nchi mbalimbali masikini katika mifumo yake ya afya. Achilia mbali ya kutokuwepo kwa hospitali na zahanati za kutosha, lakini hata hizo zilizokuwepo zina upungu mkubwa wa vifaa tiba.

Kwa kuzingatia hilo, baada ya kujua shida za ndugu zao wa Afrika hasa katika utoaji wa huduma za afya, China ilijitahidi kwa hali na mali kuhakikisha inakuwa nao bega kwa bega, kuwapunguzia mzigo kwa kuchangia vifaa mbalimbali zikiwemo mashine za kupumilia, barakoa na nyinginezo

Lakini waswahili wanasema abebwae hujikaza, serikali mbalimbali za Afrika zinapaswa kutatua changamoto zote zinazoikabili sekta ya afya. Hii ikiwa ni pamoja na kushirikisha hata wawekezaji wa ndani ya nchi kuipiga jeki sekta hiyo kwani tukumbuke kwamba sadaka huanzia nyumbani.

Afya ya mtu ni jambo la kunufaisha au kuangamiza nchi na taifa zima, kama si dunia nzima. Hasa tukichukulia jinsi maambukizi ya magonjwa mfano corona, yanavyosambaa kutoka kwa mtu mmoja hadi kwa mwingine, nchi na nchi au taifa moja hadi jingine. Hivyo tunatumai kwamba nchi mbambali duniani hasa za Afrika zitaweka mikakati ya kuboresha huduma za afya pamoja na kujiandaa endapo utalipuka ugonjwa wowote ule mkubwa ili kuepusha vifo vya watu na pia kuwafanya watu wawe na imani na mifumo yao ya afya.

CRI

  • Tags

You can share this post!

Kenya, Tanzania zalegeza masharti kuimarisha ushirikiano wa...

Maabara ya kupima Covid-19 kwenye uwanja wa ndege wa...