Na SAMMY WAWERU
WAFANYABIASHARA wa Tanzania wako huru kuwekeza nchini bila kuwekewa vikwazo vyovyote.
Rais Uhuru Kenyatta ametangaza Jumatano kwamba wawekezaji kutoka taifa hilo jirani hawatahitaji kuwa na visa wala kibali chochote kuendesha biashara humu nchini.
“Wafanyabiashara kutoka Tanzania kuanzia leo nasema mko huru kuja Kenya kuwekeza bila kuitishwa visa na kibali cha biashara,” akasema Rais Kenyatta, akihutubu katika kongamano lililoandaliwa na sekta ya biashara Kenya na Tanzania.
Hafla hiyo imeandaliwa jijini Nairobi wakati ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anafanya ziara yake ya siku mbili nchini.
“Wawekezaji kutoka Tanzania muwe huru kuja kufanya kazi hapa nchini, bora tu mheshimu sheria zinazohitajika,” akaeleza Rais Kenyatta.
Ziara ya Rais Samia ya siku mbili Kenya na inayokamilika leo, Jumatano, inalenga kuimarisha uhusiano bora wa kidiplomasia na kibiashara kati ya Kenya na Tanzania, ili kuboresha uchumi wa mataifa haya mawili.