SHANGAZI;
Nina umri wa miaka 35. Imekuwa vigumu kwangu kupata mpenzi kutokana na hali yangu ya kuogelea bila kufika ukingoni. Hali hiyo hugeuza raha ya mahaba kuwa maumivu tele. Je, nitapata wapi suluhisho?
Huba ni shughuli ya furaha na inafaa kuwafurahisha na kuwatosheleza wahusika wote wawili. Hali yako hiyo isiporekebishwa ina maana kwamba hutawahi kuwa na mpenzi wala mke. Ni muhimu utafute msaada wa daktari kwa haraka.
Mpenzi wangu aliniacha alipogundua nilikuwa nikimcheza na mwanamume mwingine. Nimegundua aliyefanya tuachane ana wanawake chungu nzima. Najuta na natamani kumrudia wa awali.
Hatua ya kumcheza mpenzi wako ilitokana na tamaa tu. Sidhani atakubali ombi lako. Lakini unaweza kujaribu kama bado hajapata mwingine. Sasa umejua umuhimu wa kuwa mwaminifu.
Nimekuwa na mpenzi kwa miaka mitatu sasa na ameamua kunioa. Tatizo ni kuwa wazazi wangu hawamfahamu na sijui kama watamkubali au la.
Mapenzi na ndoa ni suala la kibinafsi. Ni haki yako kuamua jambo lolote muhimu kuhusu maisha yako. Wazazi wako hawana wajibu wa kuamua ni nani anayefaa kuwa mume wako. Hata hivyo, ni muhimu wamjue.
Nilimuacha mpenzi wangu kwa sababu hakuwa mwaminifu. Tatizo ni kuwa bado nahangaika moyoni kwa mapenzi yake. Nimempigia simu mara nyingi nikitaka tuonane lakini anapuuza. Nifanye nini?
Unahangaisha moyo wako bure. Mwanamume huyo hakupendi, ametosheka na huyo mwingine ndio maana anapuuza simu zako. Itabidi ukubali kwamba huwezi kumpata tena na umuondoe kabisa katika mawazo yako.